Generic placeholder image

Julai, 03

Mt. TOMA MTUME
Jumatano Juma la 13 SALA ZA MCHANA

K. Ee Mungu, uje kutusaidia.
W. Ee Bwana, utusaidie hima.
Atukuzwe Baba na Mwana na Roho Mtakatifu, kama mwanzo, na sasa, na siku zote, na milele. Amina. Aleluya.

UTENZI
Ee Bwana Mbarikiwa,
Mungu Muumbaji wetu,
Vitu vyote hutakaswa
Katika Wewe, E Mungu,
Wewe waviimarisha
Hata milele vidumu.

Wenye heri, e mkono
Mtakatifu wa Mungu,
Ndiwe watakatifuza
Vitu vyote, vyote vitu,
Na upya unavitia
Wavipamba vyasitawi.

Ewe fahari tukufu,
Enzi yake Bwana Mungu,
Ndani mwako wachukua
Vyote unavyovijaza;
Na yote yanafanyika
Kadiri unavyotaka.

Usifiwe, utukuzwe
Utatu Mtakatifu,
Ujuaye kwa hakika
Na makini zako njia;
Wewe ndiwe nuru kuu
Milele inayodumu.

Kabla ya Adhuhuri
Ant.: Nendeni, mkahubiri Habari Njema ya utawala: mlipata bure; toeni bure (aleluya).

Adhuhuri
Ant.: Nipo nanyi sikuzote, hata mwisho wa nyakati (aleluya).

Baada ya Adhuhuri
Ant.: Kwa uvumilivu wenu, mtayaokoa maisha yenu (aleluya).

Zab.119:9-16 II Uaminifu kwa Sheria ya Mungu
Kijana atatunzaje mwenendo wake uwe safi?*
Kwa kuyashika maagizo yako.

Najitahidi kukutii kwa moyo wote;*
unijalie kuzishika amri zako.

Nimeshika agizo lako moyoni mwangu,*
nisije nikakukosea.

Utukuzwe, Ee Mungu!*
Unifundishe kanuni zako.

Nitazirudia kwa sauti*
sheria zako zote ulizotoa.

Nafurahi kufuata amri zako,*
kuliko kuwa na utajiri mwingi.

Nazitafakari amri zako,*
na kuyazingatia maagizo yako.

Nazifurahia kanuni zako;*
sitazisahau amri zako.

Atukuzwe Baba na Mwana*
na Roho Mtakatifu.

Kama mwanzo na sasa na siku zote*
na milele. Amina

Zab.17 Sala ya mtu mwema
Yesu alipokuwa anaishi hapa duniani, kwa kilio kikuu na machozi, alisali na kumwomba Mungu ambaye alikuwa na uwezo wa kumwokoa kutoka kifo; naye akasikilizwa (Ebr.5:7)

I
Ee Mungu, unisikilize niombapo haki zangu;/
usikilize kilio changu,*
upokee ombi langu la moyo mnyofu.

Utatoa hukumu ya kunifadhili,*
kwani wewe wajua jambo la haki.

Wewe waujua kabisa moyo wangu;/
umenijia usiku, umenichunguza;*
hukuona uovu wowote ndani yangu.

Sisemi maovu, kama wafanyavyo wengine;*
nimeitii amri yako, sikuishika njia ya wadhalimu.

Nimefuata daima njia yako;*
wala sikuiacha kamwe.

Nakuita, Ee Mungu, kwani wanisikiliza;*
unitegee sikio, uyasikilize maneno yangu.

Onyesha upendo wako mkuu,/
uwaokoe kutoka kwa adui zao,*
wale wanaokukimbilia.

Unilinde kama mboni ya jicho lako;/
unifiche kivulini mwa mabawa yako,*
mbali na mashambulio ya waovu.

Atukuzwe Baba na Mwana*
na Roho Mtakatifu.

Kama mwanzo na sasa na siku zote*
na milele. Amina

II
Adui wa hatari wanizunguka,/
hawana huruma yoyote ile;*
wamejaa maneno ya kujigamba.

Sasa wamenizingira pande zote;*
wanavizia waniangushe chini.

Wako tayari kunirarua kama simba;*
kama aviziavyo mawindo mwana-simba.

Uje, Ee Mungu, kuwakabili na kuwaporomosha.*
Kwa upanga wako uniokoe na watu waovu;

kwa mkono wako, Ee Mungu, uniokoe na watu hao,*
watu ambao huthamini riziki ya dunia hii tu.

Waadhibu kwa mateso uliyowawekea,/
yawe ya kutosha kwa watoto wao,*
wawaachie na wajukuu wao.

Lakini mimi nitakuona, kwani sikutenda ubaya;*
niamkapo nitajaa furaha kwa kukuona.

Atukuzwe Baba na Mwana*
na Roho Mtakatifu.

Kama mwanzo na sasa na siku zote*
na milele. Amina

Kabla ya Adhuhuri
Ant.: Nendeni, mkahubiri Habari Njema ya utawala: mlipata bure; toeni bure (aleluya).

Adhuhuri
Ant.: Nipo nanyi sikuzote, hata mwisho wa nyakati (aleluya).

Baada ya Adhuhuri
Ant.: Kwa uvumilivu wenu, mtayaokoa maisha yenu (aleluya).

MASOMO

Kabla ya Adhuhuri: 2Kor.5:19b-20
Mungu ametupatia ujumbe kuhusu kuwapatanisha watu naye. Basi, sisi tunamwakilisha Kristo, naye Mungu mwenyewe anatutumia sisi kuwasihi ninyi. Tunawaombeni kwa niaba ya Kristo, patanishweni na Mungu.

K. Sauti yao imeenea duniani kote (aleluya).
W. Ujumbe wao umesikika kote ulimwenguni (aleluya.)

Sala: tazama chini kabisa ukurasa huu

---
Adhuhuri: Mate.5:12a,14
Mitume walifanya miujiza na maajabu mengi kati ya watu. Idadi ya watu waliomwamini Bwana, waume kwa wake, iliongezeka zaidi na zaidi.

K. Walifuata maagizo ya Mungu (aleluya).
W. Walishika amri zake (aleluya).

Sala: tazama chini kabisa ukurasa huu

---
Baada ya Adhuhuri: Mate.5:41-42
Mitume wakatoka nje ya ule mkutano wa halmashauri, wakiwa wamejaa furaha kwa sababu walistahili kuaibishwa kwa sababu ya jina la Yesu. Wakaendelea kila siku kufundisha na kuhubiri Habari Njema ya Kristo.

K. Furahini na shangilieni, Bwana alisema (aleluya).
W. Kwa kuwa majina yenu yameandikwa mbinguni (aleluya).

SALA:
Tuombe: Baba, adhimisho letu la sikukuu ya Mtakatifu Toma mtume litupatie daima msaada na ulinzi wake. Utujalie uzima wako kutokana na imani yetu kwa Mwanao, Yesu, ambaye Toma alimkiri kuwa ni Bwana na Mungu wake. Tunaomba hayo kwa njia ya Yesu Kristo Bwana wetu.

W. Amina.

K. Tumtukuze Bwana.
(W.) tumshukuru Mungu.