Generic placeholder image

Julai, 15

MTAKATIFU BONAVENTURA
Askofu na mwalimu wa kanisa
JUMATATU JUMA LA 15 LA MWAKA
SALA ZA MCHANA

K. Ee Mungu, uje kutusaidia.
W. Ee Bwana, utusaidie hima.
Atukuzwe Baba na Mwana na Roho Mtakatifu, kama mwanzo, na sasa, na siku zote, na milele. Amina (Aleluya).

UTENZI
Bwana Mungu na wa vyote Muumba,
Ulimwengu nawe wategemezwa,
Vyote hubadilika na kuoza,
Wewe hapana, wabaki ni Mpya.

Ndiwe faraja na ya mtu kinga,
U Mwamba juu yake wa kujenga,
Ndiwe makao tulivu ya roho,
Yote hutimilika ndani yako.

Asifiwe Baba na Mwana Mungu,
Asifiwe Roho Mtakatifu;
Na utukuzwe Utatu milele,
Nguvu yetu maisha yetu yote.

Kabla ya Adhuhuri
Ant.: Baba, kama wewe ulivyonituma mimi ulimwenguni, nami nimewatuma hao ulimwenguni (aleluya).

Adhuhuri
Ant.: Mtu anayewapokea ninyi, hunipokea mimi: yeyote anayenipokea mimi, humpokea Yeye aliyenituma (aleluya).

Baada ya Adhuhuri
Ant.: Sisi twafanya kazi pamoja na Mungu; ninyi ni bustani ya Mungu, ni jengo la Mungu (aleluya).

Zab.119:89-96 XII Sheria ya Mungu hutegemewa
Nawapeni amri mpya: pendaneni; pendaneni kama nilivyowapenda ninyi (Yoh.13:34)

Neno lako, Ee Mungu, ladumu milele;*
limethibitika juu mbinguni.

Uaminifu wako wadumu vizazi vyote,*
umeiweka dunia mahali pake, nayo yadumu.

Kwa amri yako viumbe vyote vipo leo,*
kwa sababu vyote ni watumishi wako.

Kama sheria yako isingekuwa furaha yangu,*
ningalikwisha angamia kwa taabu zangu.

Sitasahau kamwe maagizo yako,*
maana kwa hayo umenipa uhai.

Mimi ni wako, unisalimishe,*
maana nimejitahidi kuzishika amri zako.

Waovu wanivizia wapate kuniua;*
lakini mimi nitazitafakari sheria zako.

Nimetambua kila kitu kina mpaka wake,*
lakini agizo lako halina mpaka.

Atukuzwe Baba na Mwana*
na Roho Mtakatifu.

Kama mwanzo na sasa na siku zote*
na milele. Amina

Zab.71 Mungu tumaini la wazee
Tumaini lenu liwaweke daima wenye furaha; muwe na saburi katika shida (Rom.12:12)

I
Ee Mungu, nimekukimbilia wewe;*
usiniache kamwe niaibike.

Kwa uadilifu wako uniopoe, uniokoe;*
unitegee sikio lako, unisalimishe!

Uwe mwamba wangu wa kukimbilia,/
ngome imara ya kunisalimisha;*
kwani wewe ni mwamba na ngome yangu.

Uniokoe, Ee Mungu wangu, mikononi mwa waovu;*
uniokoe kutoka kwa wabaya na wakatili.

Maana wewe Bwana u peke yako tegemeo langu,*
Ee Mungu, nimekutumainia tangu ujana wangu;

nimekutegemea tangu kuzaliwa kwangu,/
ndiwe uliyenitoa tumboni mwa mama yangu.*
Daima nakusifu wewe.

Kwa wengi nimekuwa mfano wa kushangaza;*
lakini wewe u kimbilio langu imara.

Kinywa changu kimejaa sifa zako,*
na utukufu wako mchana kutwa.

Wakati wa uzee usinitupe;*
niishiwapo na nguvu usiniache.

Maana adui zangu wananisema;*
wanaonivizia wanashauriana,

na kusema: “Mungu amemwacha;/
mfuateni na kumkamata,*
kwani hakuna wa kumwokoa!“

Usikae mbali nami, Ee Mungu;*
uje hima kunisaidia, Ee Mungu wangu.

Wapinzani wangu wote waaibishwe na kuangamizwa;*
wenye kunitakia mabaya wapate aibu na dhihaka.

Atukuzwe Baba na Mwana*
na Roho Mtakatifu.

Kama mwanzo na sasa na siku zote*
na milele. Amina

II
Lakini mimi nitasubiri kwa tumaini;*
tena nitakusifu zaidi na zaidi.

Mimi nitasimulia matendo yako ya haki,/
nitatangaza mchana kutwa matendo yako ya wokovu;*
ijapokuwa yanapita akili yangu.

Nitaanza na matendo yako makuu, Ee Bwana Mungu*
nitatangaza wema wako peke yako.

Ee Mungu, wewe umenifunza tangu ujana wangu*
tena na tena, natangaza matendo yako ya ajabu.

Usiniache, Ee Mungu, hata nikiwa mzee mwenye mvi,*
mpaka nivitangazie vizazi vijavyo nguvu yako.

Uwezo na uadilifu wako, Ee Mungu,*
vimefika mpaka mawinguni.

Wewe umefanya mambo makuu mno.*
Ee Mungu, ni nani aliye kama wewe?

Umeniletea taabu na shida nyingi,*
lakini utanipatia tena uzima na kuniinua.

Utaniongezea heshima yangu,*
na kunifariji tena.

Ndipo nitakusifu kwa kinanda,*
kwa sababu ya uaminifu wako, Ee Mungu wangu;

nitakuimbia sifa kwa kinubi,*
ewe Mtakatifu wa Israeli.

Nitashangilia ninapoimba sifa zako;*
nitaimba kwa moyo wote, maana umeniokoa.

Nitasimulia uadilifu wako mchana kutwa,/
maana walionitakia mabaya,*
wameona aibu na fedheha.

Atukuzwe Baba na Mwana*
na Roho Mtakatifu.

Kama mwanzo na sasa na siku zote*
na milele. Amina

Kabla ya Adhuhuri
Ant.: Baba, kama wewe ulivyonituma mimi ulimwenguni, nami nimewatuma hao ulimwenguni (aleluya).

Adhuhuri
Ant.: Mtu anayewapokea ninyi, hunipokea mimi: yeyote anayenipokea mimi, humpokea Yeye aliyenituma (aleluya).

Baada ya Adhuhuri
Ant.: Sisi twafanya kazi pamoja na Mungu; ninyi ni bustani ya Mungu, ni jengo la Mungu (aleluya).

MASOMO

Kabla ya Adhuhuri: 1Tim.4:16
Angalia sana mambo yako mwenyewe, na mafundisho yako. Endelea kufanya hayo, maana ukifanya hivyo utajiokoa mwenyewe na wale wanaokusikiliza.

K. Bwana alimchagua mtumishi wake (aleluya).
W. Alimwita awe mchungaji wa Yakobo, urithi wake (aleluya).

Sala: tazama chini kabisa ukurasa huu

---
Adhuhuri: 1Tim.1:12
Namshukuru Bwana wetu Yesu Kristo, aliyenipa nguvu kwa ajili ya kazi yangu. Namshukuru kwa kuniona mimi kuwa ni mwaminifu, akaniteua nimtumikie.

K. Sitaona aibu kutangaza Habari Njema (aleluya).
W. Uwezo wa Mungu ndio unaowaokoa watu (aleluya).

Sala: tazama chini kabisa ukurasa huu

---
Baada ya Adhuhuri: 1Tim.3:13
Wasaidizi wanaofanya kazi yao vizuri hujipatia msimamo mzuri, na wanaweza kusema bila hofu juu ya imani yao katika Kristo Yesu.

K. Kama Bwana haijengi nyumba hiyo (aleluya).
W. Wale waijengao wafanya kazi bure (aleluya).

SALA:
Tuombe: Mungu Baba Mwenyezi, leo, tunapomkumbuka Mtakatifu Bonaventura, uziangaze akili zetu kwa mafundisho yake bora, na utuwezeshe kukupenda kama yeye alivyokupenda kwa nguvu zote. Tunaomba hayo kwa njia ya Yesu Kristo Bwana wetu.

W. Amina.

K. Tumtukuze Bwana.
(W.) tumshukuru Mungu.