Generic placeholder image
Agosti 1

MT. ALFONSO MARIA WA LIGUORI
ALHAMISI JUMA LA 17 LA MWAKA
SALA ZA MCHANA

K. Ee Mungu, uje kutusaidia.
W. Ee Bwana, utusaidie hima.
Atukuzwe Baba na Mwana na Roho Mtakatifu, kama mwanzo, na sasa, na siku zote, na milele. Amina. Aleluya.

UTENZI
E Bwana Mbarikiwa,
Mungu Muumbaji wetu,
Vitu vyote hutakaswa
Katika Wewe, E Mungu,
Wewe waviimarisha
Hata milele vidumu.

Wenye heri, e mkono
Mtakatifu wa Mungu,
Ndiwe watakatifuza
Vitu vyote, vyote vitu,
Na upya unavitia
Wavipamba vyasitawi.

Ewe fahari tukufu,
Enzi yake Bwana Mungu,
Ndani mwako wachukua
Vyote unavyovijaza;
Na yote yanafanyika
Kadiri unavyotaka.

Usifiwe, utukuzwe
Utatu Mtakatifu,
Ujuaye kwa hakika
Na makini zako njia;
Wewe ndiwe nuru kuu
Milele inayodumu.

Kabla ya Adhuhuri
Ant.: Baba, kama wewe ulivyonituma mimi ulimwenguni, nami nimewatuma hao ulimwenguni (aleluya).

Adhuhuri
Ant.: Mtu anayewapokea ninyi, hunipokea mimi: yeyote anayenipokea mimi, humpokea Yeye aliyenituma (aleluya).

Baada ya Adhuhuri
Ant.: Sisi twafanya kazi pamoja na Mungu; ninyi ni bustani ya Mungu, ni jengo la Mungu (aleluya).

Zab.119:17-24 III Furaha katika sheria ya Mungu
Unifadhili mimi mtumishi wako,*
nipate kuishi na kushika agizo lako.

Uyafumbue macho yangu,*
niyaone maajabu ya sheria yako.

Mimi ni mkimbizi tu hapa duniani;*
usinifiche maagizo yako.

Roho yangu yaugua kwa hamu kubwa*
ya kutaka kujua daima hukumu zako.

Wewe wawakemea watu wenye kiburi;*
walaaniwe wanaokiuka amri zako.

Uniepushe na matusi na madharau yao,*
maana nimezishika kanuni zako.

Hata kama wakuu wanakula njama dhidi yangu,*
mimi mtumishi wako nitajifunza maagizo yako.

Amri zako ni furaha yangu;*
hunipa ushauri mwema.

Atukuzwe Baba na Mwana*
na Roho Mtakatifu.

Kama mwanzo na sasa na siku zote*
na milele. Amina

Zab.25 Kuomba uongozi na ulinzi
Tumaini hilo haliwezi kutuhadaa (Rom.5:5)

I
Kwako naja, Ee Mungu, kwa moyo wangu wote!*
Nakutumainia wewe, Ee Mungu wangu,

usiniache niaibike;*
adui zangu wasifurahie kushindwa kwangu.

Wote wale wakutegemeao hawataaibika;*
lakini wanaokuasi ovyo wataaibika.

Ee Mungu, unijulishe njia yako;*
naam, unipe mwongozo wako.

Uniongoze katika ukweli wako na kunifundisha,/
kwani wewe ni Mungu unayeniokoa;*
ninakutumainia wewe daima.

Ee Mungu, uukumbuke wema wako mkuu;/
uukumbuke na upendo wako mkuu,*
maana vimekuwako tangu milele.

Unisamehe dhambi na makosa ya ujana wangu;/
unikumbuke kadiri ya upendo wako mkuu,*
kwa ajili ya wema wako, Ee Mwenyezi.

Mungu ni mwema na mwadilifu;*
huwapa wakosefu mwongozo.

Huwaongoza wanyenyekevu katika uadilifu;*
naam, huwafundisha hao njia yake.

Mungu huwalinda kwa upendo mkuu na uaminifu,*
wale wanaozingatia matakwa ya agano lake.

Kwa heshima ya jina lako, Ee Mungu,*
unisamehe uovu wangu, kwani ni mkubwa.

Atukuzwe Baba na Mwana*
na Roho Mtakatifu.

Kama mwanzo na sasa na siku zote*
na milele. Amina

II
Kila mtu anayemcha Mungu,*
atafunzwa naye mwongozo wa kufuata.

Mtu wa namna hiyo atafanikiwa daima;*
na watoto wake watamiliki nchi.

Mungu ni msiri wa watu wanaomcha;*
yeye huwajulisha hao agano lake.

Namtazamia Mungu daima anisaidie;*
yeye peke yake ataniokoa mtegoni.

Uniangalie, Ee Mungu, unionee huruma,*
kwa sababu mimi niko peke yangu, na mnyonge.

Uniondolee mahangaiko yangu;*
uniokoe katika taabu zangu.

Uangalie unyonge wangu na dhiki yangu;*
unisamehe dhambi zangu zote.

Angalia jinsi walivyo wengi adui zangu;*
ona jinsi wanavyonichukia mno.

Uyalinde maisha yangu na kuniokoa;*
nakukimbilia wewe, usikubali niaibike.

Wema na uadilifu vinihifadhi,*
maana ninakutumainia wewe.

Ee Mungu, uwaokoe watu wako, Israeli;*
uwaokoe katika taabu zao zote.

Atukuzwe Baba na Mwana*
na Roho Mtakatifu.

Kama mwanzo na sasa na siku zote*
na milele. Amina

Kabla ya Adhuhuri
Ant.: Baba, kama wewe ulivyonituma mimi ulimwenguni, nami nimewatuma hao ulimwenguni (aleluya).

Adhuhuri
Ant.: Mtu anayewapokea ninyi, hunipokea mimi: yeyote anayenipokea mimi, humpokea Yeye aliyenituma (aleluya).

Baada ya Adhuhuri
Ant.: Sisi twafanya kazi pamoja na Mungu; ninyi ni bustani ya Mungu, ni jengo la Mungu (aleluya).

MASOMO

Kabla ya Adhuhuri: 1Tim.4:16
Angalia sana mambo yako mwenyewe, na mafundisho yako. Endelea kufanya hayo, maana ukifanya hivyo utajiokoa mwenyewe na wale wanaokusikiliza.

K. Bwana alimchagua mtumishi wake (aleluya).
W. Alimwita awe mchungaji wa Yakobo, urithi wake (aleluya).

Sala: tazama chini kabisa ukurasa huu

---
Adhuhuri: 1Tim.1:12
Namshukuru Bwana wetu Yesu Kristo, aliyenipa nguvu kwa ajili ya kazi yangu. Namshukuru kwa kuniona mimi kuwa ni mwaminifu, akaniteua nimtumikie.

K. Sitaona aibu kutangaza Habari Njema (aleluya).
W. Uwezo wa Mungu ndio unaowaokoa watu (aleluya).

Sala: tazama chini kabisa ukurasa huu

---
Baada ya Adhuhuri: 1Tim.3:13
Wasaidizi wanaofanya kazi yao vizuri hujipatia msimamo mzuri, na wanaweza kusema bila hofu juu ya imani yao katika Kristo Yesu.

K. Kama Bwana haijengi nyumba hiyo (aleluya).
W. Wale waijengao wafanya kazi bure (aleluya).

SALA:
Tuombe: Bwana Mungu, wewe huachi kamwe kulipatia Kanisa lako watakatifu wapya ili watuoneshe mifano ya kuishi kitakatifu. Utusaidie tuweze kumwiga Mtakatifu Alfonso katika bidii yake ya kuziokoa roho za watu, ili tupate kushiriki tuzo lake mbinguni. Tunaomba hayo kwa njia ya Yesu Kristo Bwana wetu.

W. Amina.

K. Tumtukuze Bwana.
(W.) tumshukuru Mungu.