Generic placeholder image

Augusti 10
MTAKATIFU LAURENT Shemasi
JUMAMOSI JUMA LA 18 LA MWAKA
SALA ZA MCHANA

K. Ee Mungu, uje kutusaidia.
W. Ee Bwana, utusaidie hima.
Atukuzwe Baba na Mwana na Roho Mtakatifu, kama mwanzo, na sasa, na siku zote, na milele. Amina. Aleluya.

UTENZI
Njoo Roho Mtakatifu,
Ndani yetu sisi uishi,
Pamoja nawe waje pia
Mungu Baba na Mungu Mwana,
Nazo zako tele neema
Njoo upate tujalia,
Zitufanye watakatifu,
Pia tuwe kitu kimoja.

Imara katika upendo
Na viwe, roho na ulimi,
Yako sifa kuitangaza
Kila mahali duniani,
Na ule upendo jalie -
Ulio mwetu mioyoni -
Mioyo mingine iwashwe
Kutokana na mwako wake.

Ee Mtukufu kabisa
Utatu ulio upendo,
Moyo wake bin-Adamu
Kwa ajili yako 'liumbwa,
Kwako Wewe na iwe sifa
Kwa wimbo usio na mwisho.
Haki yako Wewe pekee
Kwabudiwa hata milele.

Kabla ya Adhuhuri
Ant.: Bwana alimpatia ushindi baada ya mapambano makali, na akamfundisha kwamba hekima ni nguvu iliyo kuu kushinda nguvu zote (aleluya).

Adhuhuri
Ant.: Bwana alimpa taji ya heshima, na jina takatifu la utukufu (aleluya).

Baada ya Adhuhuri
Ant.: Walikwenda huku wanalia, papo hapo wanapanda mbegu (aleluya).

Zab.119:81-88 XI Sala wakati wa kudhulumiwa
Niko hoi kwa kukungojea uniokoe;*
naweka tumaini langu katika neno lako.

Macho yangu yanafifia nikingojea ulichoahidi.*
Nauliza:“Utakuja lini kunifariji?”

Nimekunjamana kama kiriba katika moshi,*
hata hivyo sijasahau amri zako.

Nitasubiri mpaka lini?*
Utawaadhibu lini wenye kunidhulumu?

Wenye kiburi, wasiojali sheria yako,*
wamenichimbia mashimo kunitega.

Amri zako zote ni za kuaminika;/
watu waongo wananidhulumu,*
tafadhali unisaidie!

Karibu wangefaulu kuniangamiza,*
lakini mimi sijavunja amri zako.

Unisalimishe kadiri ya upendo wako mkuu,*
nipate kuzingatia maagizo yako.

Atukuzwe Baba na Mwana*
na Roho Mtakatifu.

Kama mwanzo na sasa na siku zote*
na milele. Amina

Zab.61 Kuomba ulinzi
Sala ya mwadilifu atamaniye mambo ya mbinguni (Mt. Hilari)

Usikie kilio changu, Ee Mungu;*
usikilize sala yangu.

Ninakulilia ugenini humu;*
nikiwa nimevunjika moyo.

Unipeleke kwenye mwamba wa usalama,/
maana wewe ndiwe kimbilio langu,*
kinga yangu imara dhidi ya adui.

Uniruhusu nikae hemani mwako milele*
nipate usalama chini ya mabawa yako.

Ee Mungu, umezipokea nadhiri zangu,*
umenijalia mema uliyowaahidia wakuchao.

Umjalie mfalme maisha marefu,*
miaka yake iwe ya vizazi vingi.

Atawale milele mbele yako, Ee Mungu;*
mapendo na uaminifu wako vimlinde.

Hapo nitakuimbia nyimbo za sifa,*
nikizitekeleza kila siku nadhiri zangu.

Atukuzwe Baba na Mwana*
na Roho Mtakatifu.

Kama mwanzo na sasa na siku zote*
na milele. Amina

Zab.64 Sala ya kuomba ulinzi wa Mungu
Zaburi hii hasa yatualika kuyafikiria mateso ya Bwana (Mt. Augustino)

Usikie, Ee Mungu, usikilize lalamiko langu;*
unilinde maisha yangu na vitisho vya adui.

Unikinge na njama za waovu,*
na ghasia za watu wabaya.

Wananoa ndimi zao kama upanga,*
wanafyatua maneno ya ukatili kama mishale.

Toka mafichoni wanamshambulia mtu mnyofu,*
wanamshambulia ghafula bila kuogopa.

Wanashirikiana katika nia yao mbaya;/
wanapatana mahali pa kuficha mitego yao.*
Wakifikiri: “Hakuna atakayeweza kuiona!”

Hufanya njama zao na kusema:/
"Sasa tumekamilisha mpango.*
Nani atagundua hila zetu?”

Mipango ya siri imefichika moyoni mwa mtu!/
Lakini Mungu atawapiga mishale,*
na kuwajeruhi ghafula.

Atawaangamiza kwa sababu ya maneno yao;*
kila atakayewaona atatikisa kichwa.

Hapo watu wote wataogopa;/
watatangaza aliyotenda Mungu,*
na kufikiri juu ya matendo yake.

Waadilifu watafurahia aliyotenda Mungu,/
watakimbilia usalama kwake.*
Watu wote wema wataona fahari.

Atukuzwe Baba na Mwana*
na Roho Mtakatifu.

Kama mwanzo na sasa na siku zote*
na milele. Amina

Kabla ya Adhuhuri
Ant.: Bwana alimpatia ushindi baada ya mapambano makali, na akamfundisha kwamba hekima ni nguvu iliyo kuu kushinda nguvu zote (aleluya).

Adhuhuri
Ant.: Bwana alimpa taji ya heshima, na jina takatifu la utukufu (aleluya).

Baada ya Adhuhuri
Ant.: Walikwenda huku wanalia, papo hapo wanapanda mbegu (aleluya).

MASOMO

Kabla ya Adhuhuri: 1Pet.5:10-11
Mkisha teseka muda mfupi, Mungu aliye asili ya neema yote, na ambaye anawaiteni muushiriki utukufu wake wa milele katika kuungana na Kristo, yeye mwenyewe atawakamilisheni na kuwapeni uthabiti, nguvu na msingi imara. Kwake uwe uwezo milele! Amina.

K. Bwana alimpa joho la furaha (aleluya).
W. Aliweka taji ya utukufu juu ya kichwa chake (aleluya).

Sala: tazama chini kabisa ukurasa huu

---
Adhuhuri: Yak.1:12
Heri mtu anayebaki mwaminifu katika majaribu, kwani akisha stahimili, atapewa tuzo la uzima ambalo Mungu aliwaahidia wale wanaompenda.

K. Nilimtumainia Bwana (aleluya).
W. Sitaogopa matendo ya wanadamu (aleluya).

Sala: tazama chini kabisa ukurasa huu

---
Baada ya Adhuhuri: Hek.3:1-2a,3b
Roho zao wenye haki wamo mkononi mwa Mungu, wala maumivu hayatawagusa. Machoni pa watu walio wajinga walionekana kwamba wamekufa, bali wao wenyewe wamo katika amani.

K. Watarejea wakiwa wanaimba kwa furaha (aleluya).
W. Watarudi nyumbani wamechukua matita (aleluya).

SALA:
Tuombe: Bwana Mungu, ulimtia Mtakatifu Laurenti upendo mkuu hivi hata akatukuka kwa kulitumikia taifa lako maishani mwake na kwa kifodini azizi. Utusaidie tuweze kupenda kile alichokipenda yeye, na kuishi kama yeye alivyotuonesha. Tunaomba hayo kwa njia ya Yesu Kristo Bwana wetu.

W. Amina.

K. Tumtukuze Bwana.
(W.) tumshukuru Mungu.