Generic placeholder image

Agosti 14
MTAKATIFU MAXIMILIANO MARIA KOLBE Padre
JUMATANO JUMA LA 19 LA MWAKA
SALA ZA MCHANA

K. Ee Mungu, uje kutusaidia.
W. Ee Bwana, utusaidie hima.
Atukuzwe Baba na Mwana na Roho Mtakatifu, kama mwanzo, na sasa, na siku zote, na milele. Amina. Aleluya.

UTENZI
Bwana Mungu na wa vyote Muumba,
Ulimwengu nawe wategemezwa.
Vyote hubadilika na kuoza,
Wewe hapana, wabaki ni Mpуа.

Ndiwe faraja na ya mtu kinga,
U Mwamba juu yake wa kujenga,
Ndiwe makao tulivu ya roho,
Yote hutimilika ndani yako.

Asifiwe Baba na Mwana Mungu,
Asifiwe Roho Mtakatifu;.
Na utukuzwe Utatu milele,
Nguvu yetu maisha yetu yote.

Kabla ya Adhuhuri
Ant.: Baba, kama wewe ulivyonituma mimi ulimwenguni, nami nimewatuma hao ulimwenguni (aleluya).

Adhuhuri
Ant.: Mtu anayewapokea ninyi, hunipokea mimi: yeyote anayenipokea mimi, humpokea Yeye aliyenituma (aleluya).

Baada ya Adhuhuri
Ant.: Sisi twafanya kazi pamoja na Mungu; ninyi ni bustani ya Mungu, ni jengo la Mungu (aleluya).

Zab.119:105-112 XIV Sheria ya Mungu ni mwanga
Neno lako ni taa ya kuniongoza,*
na mwanga katika njia yangu.

Nimeapa na kuthibitisha kiapo changu,*
kwamba nitashika maagizo yako maadilifu.

Ee Mungu, ninateseka mno;*
unipe uhai kama ulivyoahidi.

Ee Mungu, upokee sala yangu ya shukrani;*
na unifundishe maagizo yako.

Maisha yangu yamo hatarini daima,*
lakini siisahau sheria yako.

Waovu wamenitegea mitego kuninasa,*
lakini sikiuki amri zako.

Maagizo yako ni rasilmali yangu daima;*
naam, ni furaha ya moyo wangu.

Nimekusudia kwa moyo wote*
kutimiza kanuni zako milele.

Atukuzwe Baba na Mwana*
na Roho Mtakatifu.

Kama mwanzo na sasa na siku zote*
na milele. Amina

Zab.70 Kuomba msaada
Bwana, utuokoe, tunaangamia (Mt.8:25)

Upende, Ee Mungu, upende kuniokoa;*
Ee Mungu, uje hima kunisaidia!

Waaibike na kufedheheka,*
hao wanaotaka kuniangamiza!

Warudishwe nyuma na kupata aibu,*
hao wanaofurahia maafa yangu!

Wapumbazike kwa aibu,*
hao wanaofurahia kunidhihaki!

Lakini wote wale wanaokutafuta,*
Wafurahi na kushangilia kwa sababu yako.

Wote wale wapendao nguvu yako ya kuokoa,*
waseme daima: “Mungu ni mkuu mno!"

Mimi niliye mnyonge na fukara,*
unijie hima, Ee Mungu!

Wewe ni msaada wangu, na mkombozi wangu;*
Ee Mungu, usikawie kunisaidia.

Atukuzwe Baba na Mwana*
na Roho Mtakatifu.

Kama mwanzo na sasa na siku zote*
na milele. Amina

Zab.75 Mungu hakimu
Amewashusha wenye vyeo kutoka viti vyao. vya enzi, akawakweza wanyenyekevu (Lk.1:52)

Tunakushukuru, Ee Mungu, tunakushukuru!/
Tunatangaza ukuu wako,*
na kusimulia juu ya matendo yako makuu.

"Mimi," asema Mungu, "nimeweka wakati maalum!*
Wakati huo nitatoa hukumu iliyo sawa.

Nchi ikitetemeka na vyote vilivyomo,*
mimi ndiye ninayeitegemeza misingi yake.

Nawaambia wenye kiburi: 'Acheni kujigamba!'*
na waovu: 'Msioteshe pembe za majivuno!

Msijione kuwa watu wa maana sana,*
hata kusema maneno ya kiburi.' "

Hukumu haiji kutoka mashariki au magharibi;*
wala haitoki nyikani au mlimani.

Mungu mwenyewe ndiye hakimu;*.
humshusha mmoja na kumkweza mwingine.

Mungu anashika kikombe mkononi,*
kimejaa divai kali ya hasira yake;

anaimimina, na waovu wote wanainywa;*
naam, wanainywa mpaka tone la mwisho.

Lakini mimi nitafurahi milele,*
nitamwimbia sifa Mungu wa Yakobo.

Atavunja nguvu zote za watu waovu;*
lakini nguvu za waadilifu ataziimarisha.

Atukuzwe Baba na Mwana*
na Roho Mtakatifu.

Kama mwanzo na sasa na siku zote*
na milele. Amina

Kabla ya Adhuhuri
Ant.: Baba, kama wewe ulivyonituma mimi ulimwenguni, nami nimewatuma hao ulimwenguni (aleluya).

Adhuhuri
Ant.: Mtu anayewapokea ninyi, hunipokea mimi: yeyote anayenipokea mimi, humpokea Yeye aliyenituma (aleluya).

Baada ya Adhuhuri
Ant.: Sisi twafanya kazi pamoja na Mungu; ninyi ni bustani ya Mungu, ni jengo la Mungu (aleluya).

MASOMO

Kabla ya Adhuhuri: 1Tim.4:16
Angalia sana mambo yako mwenyewe, na mafundisho yako. Endelea kufanya hayo, maana ukifanya hivyo utajiokoa mwenyewe na wale wanaokusikiliza.

K. Bwana alimchagua mtumishi wake (aleluya).
W. Alimwita awe mchungaji wa Yakobo, urithi wake (aleluya).

Sala: tazama chini kabisa ukurasa huu

---
Adhuhuri: 1Tim.1:12
Namshukuru Bwana wetu Yesu Kristo, aliyenipa nguvu kwa ajili ya kazi yangu. Namshukuru kwa kuniona mimi kuwa ni mwaminifu, akaniteua nimtumikie.

K. Sitaona aibu kutangaza Habari Njema (aleluya).
W. Uwezo wa Mungu ndio unaowaokoa watu (aleluya).

Sala: tazama chini kabisa ukurasa huu

---
Baada ya Adhuhuri: 1Tim.3:13
Wasaidizi wanaofanya kazi yao vizuri hujipatia msimamo mzuri, na wanaweza kusema bila hofu juu ya imani yao katika Kristo Yesu.

K. Kama Bwana haijengi nyumba hiyo (aleluya).
W. Wale waijengao wafanya kazi bure (aleluya).

SALA:
Tuombe: Bwana Mungu, ulimwezesha mtakatifu Maksimilian Kolbe kustahimili mateso ya kifodini na kutoa uhai wake kwa ajili ya Kristo ndani ya ndugu; twakuomba uangalie udhaifu wetu, ukatupe nguvu ya kushuhudia ukweli wako na upendo wako kwa jinsi tunavyoishi na kufa. Tunaomba hayo kwa njia ya Yesu Kristo Bwana wetu.

W. Amina.

K. Tumtukuze Bwana.
(W.) tumshukuru Mungu.