Generic placeholder image
Agosti, 24

MT. BARTOLOMAYO MTUME
JUMAMOSI JUMA LA 20 LA MWAKA
SALA ZA MCHANA

K. Ee Mungu, uje kutusaidia.
W. Ee Bwana, utusaidie hima.
Atukuzwe Baba na Mwana na Roho Mtakatifu, kama mwanzo, na sasa, na siku zote, na milele. Amina. Aleluya.

UTENZI
Baba wa milele, Mungu wa pendo,
Ambaye kwa vumbi ulituumba,
Tugeuze kwa neema ya Roho,
Tutie thamani tulio duni.

Utuandae kwa siku ya siku
Atakapokuja Kristo kwa enzi
Kutugeuza tena toka vumbi
Na miili yetu kuing'arisha.

Ee Mungu, hujaonwa, hujaguswa
Viumbe vyote vyakudhihirisha;
Mbegu ya utukufu ndani mwetu
Itachanua tutapokuona.

Kabla ya Adhuhuri
Ant.: Nendeni, mkahubiri Habari Njema ya utawala: mlipata bure; toeni bure (aleluya).

Adhuhuri
Ant.: Nipo nanyi sikuzote, hata mwisho wa nyakati (aleluya).

Baada ya Adhuhuri
Ant.: Kwa uvumilivu wenu, mtayaokoa maisha yenu (aleluya).

Zab.119:169-176 XXII Kuomba msaada
Kilio changu kikufikie, Ee Mungu!*
Unipe maarifa kadiri ya ahadi yako.

Ombi langu likufikie;*
uniokoe kama ulivyoahidi.

Nitakutolea sifa kem kem,*
maana wanifundisha kanuni zako.

Nitaimba juu ya agizo lako,*
maana amri zako zote ni za haki.

Daima uwe tayari kunisaidia,*
maana nazifuata amri zako.

Natazamia sana uniokoe, Ee Mungu;*
sheria yako ndiyo furaha yangu.

Unijalie kuishi nipate kukusifu;*
na maagizo yako yanisaidie.

Natangatanga kama kondoo aliyepotea;/
uje kunitafuta miye mtumishi wako,*
maana sikusahau maagizo yako.

Atukuzwe Baba na Mwana*
na Roho Mtakatifu.

Kama mwanzo na sasa na siku zote*
na milele. Amina

Zab.45 Utenzi wa arusi ya kifalme
Haya, haya! Bwana arusi anakuja; nendeni kumlaki (Mt.25:6)

I
Moyo wangu umejaa mawazo mema:/
namtungia mfalme shairi langu,*
ulimi wangu u tayari kama kalamu ya mwandishi mwepesi:

wewe u mzuri kuliko wanadamu wote,/
maneno yako ni fadhili tupu,*
naye Mungu amekubariki milele.

Ewe shujaa, weka upanga wako tayari;*
wewe ni mtukufu na mwenye fahari.

Songa mbele kwa ushindi, utetee haki na ukweli,*
mkono wako ukupatie ushindi mkubwa.

Mishale yako ni mikali,/
hupenya mioyo ya adui za mfalme;*
nayo mataifa huanguka chini yako.

Utawala wako ni kama wa Mungu, wadumu milele;*
wewe wawatawala watu wako kwa haki.

Wapenda uadilifu na kuchukia uovu./
Kwa hiyo Mungu, Mungu wako, amekuteua,*
na kukumiminia furaha kubwa zaidi kuliko wenzako.

Mavazi yako yanukia marashi na udi,/
wanamuziki wakuimbia katika majumba*
yaliyopambwa kwa pembe za ndovu.

Binti za wafalme ni baadhi ya wanaokulaki,/
naye malkia amesimama kulia kwako,*
amevaa mapambo ya dhahabu safi.

Atukuzwe Baba na Mwana*
na Roho Mtakatifu.

Kama mwanzo na sasa na siku zote*
na milele. Amina

II
Nawe binti, sikiliza! Nisikilize kwa makini:*
sahau sasa watu wako na jamaa zako.

Uzuri wako wamvutia mfalme:*
yeye ni bwana wako, lazima umtii.

Watu wa Turo watakuletea zawadi;*
matajiri watataka upendeleo wako.

Binti mfalme anaingia - mzuri kabisa!*
Vazi lake limefumwa kwa nyuzi za dhahabu.

Amevalia vazi la rangi nyingi,*
aongozwa kwa mfalme

akisindikizwa na wanawali wenzake,*
nao pia wanapelekwa kwa mfalme.

Kwa furaha na shangwe wanafika huko,*
na kuingia katika jumba la mfalme.

Ee mfalme, utapata watoto wengi/
watakaotawala badala ya wazee wako;*
utawafanya watawale duniani kote.

Sifa zako nitazieneza kwa vizazi vyote daima,*
nayo mataifa yatakusifu daima na milele.

Atukuzwe Baba na Mwana*
na Roho Mtakatifu.

Kama mwanzo na sasa na siku zote*
na milele. Amina

Kabla ya Adhuhuri
Ant.: Nendeni, mkahubiri Habari Njema ya utawala: mlipata bure; toeni bure (aleluya).

Adhuhuri
Ant.: Nipo nanyi sikuzote, hata mwisho wa nyakati (aleluya).

Baada ya Adhuhuri
Ant.: Kwa uvumilivu wenu, mtayaokoa maisha yenu (aleluya).

MASOMO

Kabla ya Adhuhuri: 2Kor.5:19b-20
Mungu ametupatia ujumbe kuhusu kuwapatanisha watu naye. Basi, sisi tunamwakilisha Kristo, naye Mungu mwenyewe anatutumia sisi kuwasihi ninyi. Tunawaombeni kwa niaba ya Kristo, patanishweni na Mungu.

K. Sauti yao imeenea duniani kote (aleluya).
W. Ujumbe wao umesikika kote ulimwenguni (aleluya.)

Sala: tazama chini kabisa ukurasa huu

---
Adhuhuri: Mate.5:12a,14
Mitume walifanya miujiza na maajabu mengi kati ya watu. Idadi ya watu waliomwamini Bwana, waume kwa wake, iliongezeka zaidi na zaidi.

K. Walifuata maagizo ya Mungu (aleluya).
W. Walishika amri zake (aleluya).

Sala: tazama chini kabisa ukurasa huu

---
Baada ya Adhuhuri: Mate.5:41-42
Mitume wakatoka nje ya ule mkutano wa halmashauri, wakiwa wamejaa furaha kwa sababu walistahili kuaibishwa kwa sababu ya jina la Yesu. Wakaendelea kila siku kufundisha na kuhubiri Habari Njema ya Kristo.

K. Furahini na shangilieni, Bwana alisema (aleluya).
W. Kwa kuwa majina yenu yameandikwa mbinguni (aleluya).

SALA:
Tuombe: Bwana Mwenyezi na Baba, utuimarishe katika imani ile ambayo ilimfanya Mtakatifu Bartolomayo ajitoe kabisa nafsi yake kwa ajili ya Kristo Mwanao. Kwa maombezi yake, ulijalie Kanisa lako lipate kuwa sakramenti ya wokovu kwa ajili ya mataifa yote duniani. Tunaomba hayo kwa njia ya Yesu Kristo Bwana wetu.

W. Amina.

K. Tumtukuze Bwana.
(W.) tumshukuru Mungu.