Generic placeholder image

Oktoba 4
MTAKATIFU FRANSIS WA ASSISI
IJUMAA JUMA LA 26 LA MWAKA
SALA ZA MCHANA

K. Ee Mungu, uje kutusaidia.
W. Ee Bwana, utusaidie hima.
Atukuzwe Baba na Mwana na Roho Mtakatifu, kama mwanzo, na sasa, na siku zote, na milele. Amina. Aleluya.

UTENZI
Njoo Roho Mtakatifu,
Ndani yetu sisi uishi,
Pamoja nawe waje pia
Mungu Baba na Mungu Mwana,
Nazo zako tele neema
Njoo upate tujalia,
Zitufanye watakatifu,
Pia tuwe kitu kimoja.

Imara katika upendo
Na viwe, roho na ulimi,
Yako sifa kuitangaza
Kila mahali duniani,
Na ule upendo jalie -
Ulio mwetu mioyoni -
Mioyo mingine iwashwe.
Kutokana na mwako wake.

Ee Mtukufu kabisa
Utatu ulio upendo,
Moyo wake bin-Adamu
Kwa ajili yako 'liumbwa,
Kwako Wewe na iwe sifa
Kwa wimbo usio na mwisho,
Haki yako Wewe pekee
Kwabudiwa hata milele.

Kabla ya Adhuhuri
Ant.: Mtu ye yote akilitii neno la Kristo, upendo wa Mungu hukamilika ndani yake (aleluya).

Adhuhuri
Ant.: Mtu anayefanya atakavyo Baba yangu aliye mbinguni, ataingia katika ufalme wa mbinguni (aleluya).

Baada ya Adhuhuri
Ant.: Wewe peke yako, Mungu, umeviona vitu ambavyo umewatayarishia wale wanaokutumainia (aleluya).

Zab.119:73-80 Uadilifu wa sheria ya Mungu
Wewe mwenyewe umeniumba na kunitegemeza;*
unijalie akili nijifunze maagizo yako.

Wakuchao wataniona na kufurahi,*
kwa sababu nimelitumainia neno lako.

Najua kwamba hukumu zako ni adili, Ee Mungu,*
na kwamba umeniadhibu kwani wewe ni mwaminifu.

Upendo wako mkuu wanifariji,*
kama ulivyoniahidi mimi mtumishi wako.

Unionee huruma nipate kuishi,*
maana sheria yako ni furaha yangu.

Wenye kiburi waaibike maana wamenifanyia hila,*
lakini mimi nitayatafakari maagizo yako.

Wote wakuchao na waje kwangu,*
wapate kuzijua kanuni zako.

Nizishike amri zako kikamilifu,*
nisije nikaaibishwa.

Atukuzwe Baba na Mwana*
na Roho Mtakatifu.

Kama mwanzo na sasa na siku zote*
na milele. Amina

Zab.59:1-4,9-10,16-17 Sala ya kuomba ulinzi wa Mungu
Maneno haya ya Mwokozi na yawafundishe watu wote kumtumainia Baba yake kama watoto wachaji (Eusebius wa Kaisaria)

Ee Mungu wangu, uniokoe na adui zangu;*
unikinge na hao wanaonishambulia.

Uniokoe na hao watu waovu;*
unisalimishe na hao wauaji!

Tazama! Wananivizia waniue;*
watu wakatili wanajiunga dhidi yangu.

Bila ya kosa, hatia au dhambi yangu,/
wanakimbia, Ee Mungu, kujiweka tayari.*
Uinuke, Ee Mungu, ukatazame na kunisaidia!

Nitakuimbia sifa, ewe uliye nguvu yangu;*
maana wewe, Ee Mungu, ni ngome yangu.

Mungu wangu atanijia kwa upendo wake mkuu,*
ataniwezesha mpaka niwaone adui zangu wameshindwa.

Lakini mimi nitaimba sifa za nguvu yako;*
nitashangilia upendo wako mkuu asubuhi;

maana wewe umekuwa ngome yangu imara,*
na kimbilio langu wakati wa shida.

Ewe uliye nguvu yangu, nitakusifu;/
Ee Mungu, wewe u ngome yangu;*
Mungu unayenipenda!

Atukuzwe Baba na Mwana*
na Roho Mtakatifu.

Kama mwanzo na sasa na siku zote*
na milele. Amina

Zab.60 Ushindi baada ya kushindwa
Ulimwenguni mtapata masumbuko; lakini. jipeni moyo! Mimi nimeushinda ulimwengu(Yoh.16:33)

Ee Mungu, umetutupa na kututawanya*
umewaka hasira, tafadhali uturudishe.

Umeitetemesha nchi na kuipasua;*
uzibe nyufa zake kwani inabomoka.

Umewatwika watu wako mateso;*
tunayumbayumba kama waliolewa mvinyo.

Umewaashiria wale wanaokuheshimu,*
wapate kuukwepa mshale.

Uwasalimishe hao watu uwapendao;*
utuokoe kwa mkono wako, na kutusikiliza.

Mungu amesema kutoka patakatifu pake:/
"Sasa nitakwenda kwa shangwe kuigawa Shekemu;*
bonde la Sukoti nitaligawa sehemu sehemu.

Gileadi ni yangu, na Manase ni yangu;/
Efraimu ni kofia yangu ya chuma,*
na Yuda ni fimbo yangu ya enzi.

Moabu ni kama bakuli langu la kunawia,/
kiatu changu nitakitupia Edomu ili kuimiliki.*
Nitapiga kelele ya ushindi juu ya Filistia.“

Ni nani atakayenipeleka kwenye mji wa ngome?*
Ni nani atakayeniongoza mpaka Edomu?

Je, umetuacha kabisa, Ee Mungu?*
Je, huendi tena na majeshi yetu?

Utupatie msaada dhidi ya adui zetu,*
maana msaada wa binadamu haufai kitu.

Tutashinda, Mungu akiwa upande wetu,*
yeye atawaponda adui zetu.

Atukuzwe Baba na Mwana*
na Roho Mtakatifu.

Kama mwanzo na sasa na siku zote*
na milele. Amina

Kabla ya Adhuhuri
Ant.: Mtu ye yote akilitii neno la Kristo, upendo wa Mungu hukamilika ndani yake (aleluya).

Adhuhuri
Ant.: Mtu anayefanya atakavyo Baba yangu aliye mbinguni, ataingia katika ufalme wa mbinguni (aleluya).

Baada ya Adhuhuri
Ant.: Wewe peke yako, Mungu, umeviona vitu ambavyo umewatayarishia wale wanaokutumainia (aleluya).

MASOMO

Kabla ya Adhuhuri: Gal.6:8
Apandaye katika tamaa za kidunia, atavuna humo uharibifu; lakini akipanda katika Roho, atavuna kutoka kwa Roho uzima wa milele.

K. Bwana huwaongoza wanyenyekevu katika njia inayohusika (aleluya).
W. Huwafundisha maskini njia yake (aleluya).

Sala: tazama chini kabisa ukurasa huu

---
Adhuhuri: 1Kor.9:26
Ndivyo, basi, ninavyopiga mbio nikiwa na nia ya kushinda; ndivyo ninavyopigana, na si kama bondia anayetupa ngumi zake hewani. Naupa mwili mazoezi magumu, na kuutia katika nidhamu kamili.

K. Bwana, ana heri mtu unayemfunza (aleluya).
W. Unamfundisha kwa sheria yako (aleluya).

Sala: tazama chini kabisa ukurasa huu

---
Baada ya Adhuhuri: Filp.4:8,9
Ndugu zangu, jazeni fikra zenu kwa mambo mema na yanayostahili kusifiwa; mambo ya kweli, bora, ya haki, safi, ya kupendeza na ya heshima. Naye Mungu anayetujalia amani atakuwa pamoja nanyi.

K. Wale wanaokutumaini, na washangilie (aleluya).
W. Watafurahi milele; nawe utakaa kati yao (aleluya).

SALA:
Tuombe: Bwana Mungu, ulimfanya Mtakatifu Fransis wa Assisi afanane na Kristo katika ufukara na unyenyekevu wake. Utusaidie tuweze kutembea katika njia zake ili, kwa furaha na upendo, tumfuate Kristo Mwanao, na tuungane nawe. Tunaomba hayo kwa njia ya Yesu Kristo Bwana wetu.

W. Amina.

K. Tumtukuze Bwana.
(W.) tumshukuru Mungu.