JUMAMOSI JUMA 29 LA MWAKA WA 2
MASOMO
SOMO: Efe.4:7-16
Kila mmoja wetu alipewa neema kwa kadiri ya kipimo cha kipawa chake Kristo. Hivyo husema, Alipopaa
juu aliteka mateka, Akawapa wanadamu vipawa. Basi neno hilo, Aliopaa, maana yake nini kama siyo
kusema kwamba yeye naye alishuka mpaka pande zilizo chini, za nchi? Naye aliyeshuka ndiye yeye
aliyepaa; juu sana kupita mbingu zote, ili avijaze vitu vyote. Naye alitoa wengine kuwa mitume;
na wengine kuwa manabii; na wengine kuwa wainjilisti; na wengine kuwa wachungaji na waalimu; kwa
kusudi la kuwakamilisha watakatifu, hata kazi ya huduma itendeke, hata mwili wa Kristo ujengwe;
hata na sisi sote tutakapoufikia umoja wa Imani na kumfahamu sasa Mwana wa Mungu, hata kuwa mtu
mkamilifu, hata kufika kwenye cheo cha kimo cha utimilifu wa Kristo. Tusiwe tena watoto wachanga,
tukitupwa huku na huku, na kuchukuliwa na kila upepo wa elimu, kwa hila ya watu, kwa ujanja,
tukizifuata njia za udanganyifu. Lakini tuishike kweli katika upendo na kukua hata tumfikie yeye
katika yote, yeye aliye kichwa, Kristo. Katika yeye mwili wote ukiungamanishwa na kushikanishwa
kwa msaada wa kila kiungo, kwa kadiri ya utendaji wa kila sehemu moja moja, huukuza mwili upate
kujijenga wenyewe katika upendo.
WIMBO WA KATIKATI: Zab.122:1-5(K)1
1. Nalifurahi waliponiambia,
Na twende nyumbani kwa Bwana.
Miguu yetu imesimama
Ndani ya malango yako, Ee Yerusalemu.
(K) Nalifurahi waliponiambia, na twende nyumbani kwa Bwana.
2. Ee Yerusalemu uliyejengwa
Kama mji ulioshikamana,
Huko ndiko waliopanda kabila,
Kabila za Bwana. (K)
3. Ushuhuda kwa Israeli,
Walishukuru jina la Bwana.
Maana huko viliwekwa viti vya hukumu,
Viti vya enzi vya mbari ya Daudi. (K)
SHANGILIO: 2Tim.1:10
Aleluya, aleluya!
Mwokozi wetu Yesu Kristo alibatili mauti, na kuufunua uzima na kutokuharibika kwa Injili.
Aleluya!
INJILI: Lk.13:1-9
Wakati huo walikuwapo watu waliompasha Yesu habari ya Wagalilaya wale ambao Pilato alichanganya
damu yao na dhabihu zao. Akawajibu akawaambia, Je! Mwadhani ya kwamba Wagalilaya hao walikuwa wenye
dhambi kuliko Wagalilaya wote, hata wakapatwa na mambo hayo? Nawaambia, Sivyo; lakini msipotubu,
ninyi nyote mtaangamia vivyo hivyo. Au wale kumi na wanane, walioangukiwa na mnara huko Siloamu,
ukawaua mwadhani ya kwamba wao walikuwa wakosaji kuliko watu wote waliokaa Yerusalemu? Nawaambia,
Sivyo; lakini msipotubu, ninyi nyote mtaangamia vivyo hivyo. Akanena mfano huu; Mtu mmoja alikuwa
na mtini umepandwa katika shamba lake la mizabibu; akaenda akitafua matunda juu yake, asipate.
Akamwambia mtunzaji wa shamba la mizabibu, Tazama, miaka mitatu hii naja nikitafuta matunda juu
ya mtini huu, nisipate kitu; uukate, mbona hata nchi unaiharibu? Akajibu akamwambia, Bwana, uuache
mwaka huu nao, hata niupalilie, niutilie samadi; nao ukizaa matunda baadaye, vema! La, usipozaa,
ndipo uukate.