JUMATANO JUMA 14 LA MWAKA WA 2
MASOMO

SOMO: Hos.10:1-3,7-8,12
Bwana asema hivi: Israeli ni mzabibu, utoao matunda yake; kwa kadiri ya wingi wa matunda yake; kwa kadiri iyo hiyo ameongeza madhabahu zake; kwa kadiri ya wema wa nchi yake, kwa kadiri hiyo hiyo wamefanya nguzo nzuri. Moyo wao umegawanyika; sasa wataonekana kuwa na hatia; yeye atazipiga madhabahu zao, ataziharibu nguzo zao. Yakini sasa watasema, Hatuna mfalme; kwa maana hatumchi Bwana; na mfalme huyu je! Aweza kututendea nini? Katika habari za Samaria, mfalme wake amekatiliwa mbali, kama povu usoni pa maji. Israeli, pataharibika; mwiba na mbigili itamea juu ya madhabahu zake; nao wataiambia milima, Tusitirini; na vilima, tuangukeni. Jipandieni katika haki, vuneni kwa fadhili; uchimbueni udongo wa mashamba yenu; kwa maana wakati umewadia wa kumtafuta Bwana, hata atakapokuja na kuwanyeshea haki.

WIMBO WA KATIKATI: Zab.105:2-7(K)4
1. Mwimbieni, mwimbieni kwa zaburi,
Zitafakarini ajabu zake zote.
Jisifuni kwa jina lake takatifu,
Na ufurahi moyo wao wamtafutao Bwana.

(K) Siku zote mtafuteni uso wake Bwana.

2. Mtakeni Bwana na nguvu zake,
Utafuteni uso wake siku zote.
Zikumbukeni ajabu zake alizozifanya.
Miujiza yake na hukumu za kinywa chake. (K)

3. Enyi wazao wa Ibrahimu, mtumishi wake;
Enyi wana wa Yakobo, wateule wake.
Yeye, Bwana, ndiye Mungu wetu;
Duniani mwote mna hukumu zake. (K)

SHANGILIO: 2Tim.1:10
Aleluya, aleluya!
Mwokozi wetu Yesu Kristo alibatili mauti, na kuufunua uzima na kutokuharibika kwa Injili.
Aleluya!

INJILI: Mt.10:1-7
Yesu aliwaita wanafunzi wake kumi na wawili, akawapa amri juu ya pepo wachafu, wawatoe, na kupoza magonjwa yote na udhaifu wa kila aina. Na majina ya hao mitume kumi na wawili ni haya; Wa kwanza Simoni aliyeitwa Petro, na Andrea nduguye; Yakobo wa Zebedayo, na Yohane nduguye; Filipo, na Bartholomayo; Tomaso, na Mathayo mtoza ushuru; Yakobo wa Alfayo, na Thadayo; Simoni Mkananayo, na Yuda Iskariote, naye ndiye mwenye kumsaliti. Hao Thenashara Yesu aliwatuma, akawaagiza, akisema. Katika njia ya Mataifa msiende, wala katika mji wowote wa Wasamaria msiingie. Afadhali shikeni njia kuwaendea kondoo waliopotea wa nyumba ya Israeli. Na katika kuenenda kwenu, hubirini, mkisema, Ufalme wa mbinguni umekaribia.