JUMATANO JUMA 21 LA MWAKA WA 2
MASOMO
SOMO: 2The.3:6-10,16-18
Ndugu, twawaagiza katika jina la Bwana Yesu Kristo, jitengeni nafsi zenu na kila ndugu aendaye
bila utaratibu, wala si kwa kufuata mapokeo mliyoyapokea kwetu. Mwajua wenyewe jinsi iwapasavyo
kutufuata; kwa sababu hatukuenda bila utaratibu kwenu; wala hatukula chakula kwa mtu ye yote
bure; bali kwa taabu na masumbufu, usiku na mchana tulitenda kazi, ili tusimlemee mtu wa kwenu
awaye yote. Si kwamba hatuna amri, lakini makusudi tufanye nafsi zetu kuwa kielelezo kwenu,
mtufuate. Kwa kuwa hata wakati ule tulipokuwapo kwenu tuliwaagiza neno hili, kwamba ikiwa mtu
hataki kufanya kazi, basi, asile chakula. Sasa, Bwana wa amani mwenyewe na awape amani daima
kwa njia zote. Bwana awe pamoja nanyi nyote. Salamu zangu mimi Paulo, kwa mkono wangu mwenyewe.
Hii ndiyo alama katika kila waraka, ndio mwandiko wangu. Neema ya Bwana wetu Yesu Kristo na
iwe pamoja nanyi nyote.
WIMBO WA KATIKATI: Zab.128:1-2,4-5(K)1
1. Heri kila mtu amchaye Bwana,
Aendaye katika njia yake.
Taabu ya mikono yako hakika utaila;
Utakuwa heri, na kwako kwema.
(K) Heri kila mtu amchaye Bwana
2. Tazama, atabarikiwa hivyo, yule amchaye Bwana.
Bwana akubariki toka Sayuni;
Uone uheri wa Yerusalemu siku zote za maisha yako; (K)
SHANGILIO:
Aleluya, aleluya!
Mimi ndimi nuru ya ulimwengu, asema Bwana, yeye anifuataye hatakwenda gizani kamwe,
bali atakuwa na nuru ya uzima.
Aleluya!
INJILI: Mt.23:27-32
Yesu alisema, Ole wenu, waandishi na Mafarisayo, wanafiki! Kwa kuwa mmefanana na makaburi
yaliyopakwa chokaa, nayo kwa nje yaonekana kuwa mazuri, bali ndani yamejaa mifupa ya wafu,
na uchafu wote. Vivyo hivyo ninyi nanyi, kwa nje mwaonekana na watu kuwa wenye haki, bali
ndani mmejaa unafiki na maasi. Ole wenu, waandishi na Mafarisayo, wanafiki! Kwa kuwa mnayajenga
makaburi ya manabii, na kuyapamba maziara ya wenye haki, na kusema, Kama sisi tungalikuwako
zamani za baba zetu, hatungalishirikiana nao katika damu ya manabii. Hivi mwajishuhudia
wenyewe, ya kwamba ninyi ni wana wao waliowaua manabii. Kijazeni basi kipimo cha baba zenu.