JUMATATU JUMA 15 LA MWAKA WA 2
MASOMO
SOMO: Isa.1:10-17
Lisikieni neno la Bwana, enyi waamuzi wa Sodoma; tegeni masikio msikie sheria ya Mungu wetu, enyi
watu wa Gomora. Huu wingi wa sadaka zenu mnazonitolea una faida gani? Asema Bwana. Nimejaa mafuta
ya kafara za kondoo waume, na mafuta ya wanyama walionona; nami siifurahii damu ya ng'ombe wala ya
wana-kondoo wala ya mbuzi waume. Mjapo ili kuonekana mbele zangu, ni nani aliyetaka neno hili
mikononi mwenu, kuzikanyaga nyua zangu? Msilete tena matoleo ya ubatili; uvumba ni chukizo kwangu;
mwezi mpya na sabato, kuita makutano; siyawezi maovu hayo na makutano ya ibada. Sikukuu zenu za
mwezi mpya na karamu zenu zilizoamriwa, nafsi yangu yazichukia; mambo hayo yanilemea; nimechoka
kuyachukua. Nanyi mkunjuapo mikono yenu, nitaficha macho yangu nisiwaone; naam, mwombapo maombi
mengi, sitasikia; mikono yenu imejaa damu. Jiosheni, jitakaseni; ondoeni uovu wa matendo yenu usiwe
mbele za macho yangu; acheni kutenda mabaya; jifunzeni kutenda mema; takeni hukumu na haki;
wasaidieni walioonewa; mpatieni yatima haki yake; mteteeni mjane.
WIMBO WA KATIKATI: Zab.50:8-9,16-17,21,23(K)23
1. Sitakukemea kwa ajili ya dhabihu zako,
Na kafara zako ziko mbele zangu daima.
Sitatwaa ng’ombe katika nyumba yako,
Wala beberu katika mazizi yako.
(K) Nitamwonesha wokovu wa Mungu.
2. Una nini wewe kuitangaza sheria yangu,
Na kuliweka agano langu kinywani mwako?
Maana wewe umechukia maonyo,
Na kuyatupa maneno yangu nyuma yako. (K)
3. Ndivyo ulivyofanya, nami nikanyamaza,
Ukadhani ya kuwa Misri ni kama wewe.
Atoaye ya kuwa Misri ni kama wewe.
Atoaye dhabihu za kushukuru ndiye anayenitukuza.
Nitamwoneshsa wokovu wa Mungu. (K)
SHANGILIO:
Aleluya, aleluya!
Ee Bwana unijulishe njia zako, unifundishe mapito yako.
Aleluya!
INJILI: Mt.10:34-11:1
Yesu aliwafundisha mitume wake: Msidhani ya kuwa nimekuja kuleta amani duniani; la! Sikuja
kuleta amani, bali upanga. Kwa maana nalikuja kumfitini mtu na babaye, na binti na mamaye,
na mkwe na mkwe mtu; na adui za mtu ni wale wa nyumbani mwake. Apendaye baba au mama kuliko
mimi, hanistahili; wala apendaye mwana au binti kuliko mimi, hanistahili. Wala mtu asiyechukua
msalaba wake akanifuata, hanistahili. Mwenye kuiona nafsi yake ataipoteza; naye mwenye kuipoteza
nafsi yake kwa ajili yangu ataiona. Awapokeaye ninyi, anipokea mimi; naye anipokeaye mimi, ampokea
yeye aliyenituma. Ampokeaye nabii kwa kuwa ni nabii, atapata thawabu ya nabii; naye ampokeaye
mwenye haki kwa kuwa ni mwenye haki, atapata thawabu ya mwenye haki. Na mtu awaye yote atakayemnywesha
mmojawapo wa wadogo hawa ngaa kikombe cha maji ya baridi, kwa kuwa ni mwanafunzi, amin, nawaambia,
haitampotea kamwe thawabu yake. Ikawa Yesu alipokwisha kuwaagiza wanafunzi wake kumi na wawili,
alitoka huko kwenda kufundisha na kuhubiri katika miji yao.