JUMATATU JUMA 21 LA MWAKA WA 2
MASOMO
SOMO: The.1:1-5,11-12
Paulo, na Silwano, na Timotheo, kwa kanisa la Wathesalonike, lililo katika Mungu Baba yetu,
na Bwana Yesu Kristo. Neema na iwe kwenu na amani zitokazo kwa Mungu Baba, na kwa Bwana Yesu
Kristo. Ndugu, imetupasa kumshukuru Mungu siku zote kwa ajili yenu, kama ilivyo wajibu, kwa
kuwa imani yenu inazidi sana, na upendo wa kila mtu kwenu kwa mwenzake umekuwa mwingi. Hata
na sisi wenyewe twaona fahari juu yenu katika makanisa ya Mungu kwa ajili ya saburi yenu, na
imani mliyonayo katika adha zenu zote na dhiki mnazostahimili. Ndiyo ishara hasa ya hukumu
iliyo haki ya Mungu, ili mhesabiwe kuwa mwastahili kuingia ufalme wa Mungu, ambao kwa ajili
yake mnateswa. Kwa hiyo twawaombea ninyi siku zote, ili Mungu wetu awahesabu kuwa mmekustahili
kuitwa kwenu, akatimiza kila haja ya wema na kila kazi ya imani kwa nguvu; jina la Bwana wetu
Yesu litukuzwe ndani yenu, nanyi ndani yake, kwa neema ya Mungu wetu na ya Bwana Yesu Kristo.
WIMBO WA KATIKATI: Zab.96:1-5(K)3
1. Mwimbieni Bwana wimbo mpya,
Mwimbieni Bwana, nchi yote.
Mwimbieni Bwana, libarikini jina lake.
(K) Wahubirini mataifa habari za utukufu wake, na watu wote habari za maajabu yake.
2. Tangazeni wokovu wake siku kwa siku.
Wahubirini mataifa habari za utukufu wake,
Na watu wote habari za maajabu yake. (K)
3. Kwa kuwa Bwana ni mkuu mwenye kusifiwa sana.
Na wa kuhofiwa kuliko miungu yote.
Maana miungu yote ya watu si kitu,
Lakini Bwana ndiye aliyezifanya mbingu. (K)
SHANGILIO: Zab.147:12,15
Aleluya, aleluya!
Msifu Bwana, Ee Yerusalemu, huipeleka amri yake juu ya nchi.
Aleluya!
INJILI: Mt.23:13-22
Yesu aliwaambia makutano na wafuasi wake: Ole wenu waandishi na Mafarisayo, wanafiki! Kwa
kuwa mnawafungia watu ufalme wa mbinguni; ninyi wenyewe hamwingii, wala wanaoingia hamwaachi
waingie. Ole wenu waandishi na Mafarisayo, wanafiki! Kwa kuwa mnazunguka katika bahari na nchi
kavu ili kumfanya mtu mmoja kuwa mwongofu; na akiisha kufanyika, mnamfanya kuwa mwana wa
jehanumu mara mbili zaidi kuliko ninyi wenyewe. Ole wenu viongozi vipofu, ninyi msemao, Mtu
atakayeapa kwa hekalu, si kitu; bali mtu atakayeapa kwa dhahabu ya hekalu, amejifunga.
Wapumbavu ninyi na vipofu; maana ni ipi iliyo kubwa, ile dhahabu, au ile hekalu liitakasalo
dhahabu? Tena, Mtu atakayeapa kwa madhabahu, si kitu; bali mtu atakayeapa kwa sadaka iliyo
juu yake, amejifunga. Vipofu ninyi; maana ni ipi iliyo kubwa, ile sadaka, au ile madhabahu
iitakasayo sadaka? Basi yeye aapaye kwa madhabahu, huapa kwa hiyo, na kwa vitu vyote vilivyo
juu yake. Naye aapaye kwa hekalu, huapa kwa hilo, na kwa yeye akaaye ndani yake. Naye aapaye
kwa mbingu, huapa kwa kiti cha enzi cha Mungu, na kwa yeye aketiye juu yake.