NJIA YA MSALABA
Tufwate njia ya msalaba,
Tuifwate mpaka Kalvario,
Tusimamepo bila haya,
Msalaba, Msalaba, huponya roho.
Kwa jina la Baba, na la Mwana, na la Roho Mtakatifu: Amina.
Sala mbele ya Altare
Ee Mkombozi wangu, nimekuja leo kufuata njia ile uliyoshika siku ya kufa sadaka yetu.
Nimetubu dhambi zangu zote; ninataka kugeuza mwendo wangu; ninaomba kwako niwapatie roho
za waamini marehemu waliomo toharani, rehema zote zilizotolewa na Kanisa kwa njia
ya msalaba. Nawe Maria Bikira mtakatifu, uliyefuata njia ile nyuma ya mwanao Yesu,
uniangalie kwa wema, unitie moyo mkuu, nisipende dhambi tena, nikivumilia kazi na Usumbufu
na mateso na matukano yatakayonipata.
I
Umekosa nini we Yesu
Kushtakiwa bure kwa Pilato
Wenye kustahili hukumu
Si wewe, si wewe Bwana, ni sisi.
KITUO CHA KWANZA
Yesu anahukumiwa afe
- Ee Yesu tunakuabudu, tunakushukuru.
- Kwa kuwa umewakomboa watu kwa msalaba wako mtakatifu.
Pilato anamkuhumu Yesu ingawa haoni kosa lake, anawaogopa Wayahudi. Anabembeleza urafiki
wa Kaisari. Ee Yesu usiye na kosa, hata mimi ningeweza kutenda mema mengi, lakini naogopa
macho ya wenzangu, na maneno yao. Ee Bwana, niimarishe utashi wangu, nijitegemee katika
kushika madaraka yangu.
Baba yetu uliye mbinguni, jina lako litukuzwe. Ufalme wako ufike. Utakalo
lifanyike duniani kama mbinguni. Utupe leo mkate wetu wa kila siku. Utusamehe makosa
yetu, kama tunavyowasamehe na sisi waliotukosea. Usitutie katika kishawishi, lakini
utuopoe maovuni. Amina.
Salamu, Maria, umejaa neema; Bwana yu nawe, umebarikiwa kuliko wanawake wote,
na Yesu, mzao wa tumbo lako, amebarikiwa. Maria mtakatifu, Mama wa Mungu, utuombee
sisi wakosefu, sasa na saa ya kufa kwetu. Amina.
Atukuzwe Baba, na Mwana, na Roho Mtakatifu, kama mwanzo na sasa na siku zote na
milele. Amina
K. Ee Bwana utuhurumie
W. Utuhurumie.
k. Roho za waamini wapate rehema kwa Mungu, wapumzike kwa amani.
W. Amina.
II
Ole msalaba huo mzito
Apagazwa Mwana mpenzi wa Mungu
Mwili waenea mateso
Alipa, alipa madhambi yetu.
KITUO CHA PILI
Yesu anapokea msalaba
- Ee Yesu tunakuabudu, tunakushukuru.
- Kwa kuwa umewakomboa watu kwa msalaba wako mtakatifu.
Yesu anakubali kuupokea msalaba kwa ajili ya wokovu wa watu. Ndivyo alivyonifundisha moyo
wa sadaka, moyo wa kujitolea na kujisahau kwa ajili ya wengine. Ee Yesu wangu mkarimu, mimi
pia ninao msalaba wangu: jirani zangu, mwenzangu wa ndoa, watoto, wazazi wangu, kazi zangu,
joto, baridi, njaa, kiu, vishawishi, magonjwa na matatizo mengine ya maisha, wajibu wangu
kwa Mungu, kwa umma na kwa Kanisa. Hayo yote ni msalaba. Unipe ukarimu wako ee Yesu niyapokee
bila kunung'unika, na kuyabeba vyema.
Baba yetu...
Salamu Maria...
Atukuzwe Baba...
K. Ee Bwana utuhurumie
W. Utuhurumie.
k. Roho za waamini wapate rehema kwa Mungu, wapumzike kwa amani.
W. Amina.
III
Ona Muumba mbingu na nchi
Yupo chini mzigo wamwelemea
Na mtu kiumbe chake kwa ukali
Ampiga, ampiga bila huruma.
KITUO CHA TATU
Yesu anaanguka mara ya kwanza
- Ee Yesu tunakuabudu, tunakushukuru.
- Kwa kuwa umewakomboa watu kwa msalaba wako mtakatifu.
Yesu amedhoofika sana, anaanguka chini, kisha anasimama, anaendelea na safari ya ukombozi.
Ee Yesu uliyeanguka chini ya msalaba kwa ajili ya udhaifu ukasimama tena; usiniache
katika tamaa nikianguka dhambini, bali nisimame mara moja, nikufuate.
Baba yetu...
Salamu Maria...
Atukuzwe Baba...
K. Ee Bwana utuhurumie
W. Utuhurumie.
k. Roho za waamini wapate rehema kwa Mungu, wapumzike kwa amani.
W. Amina.
IV
Huko njiani we Maria
Waonaje hali ya mwanao
Ni damu tupu na vidonda
Machozi, machozi yamfumba macho.
KITUO CHA NNE
Yesu anakutana na Mama yake
- Ee Yesu tunakuabudu, tunakushukuru.
- Kwa kuwa umewakomboa watu kwa msalaba wako mtakatifu.
Wote wawili mama na mwanae wanaumia sana moyoni kwa ajili ya dhambi zangu.
Ee Yesu Mwana wa Maria, unitilie moyoni mwangu upendo na ibada kwa Bikira Maria:
unijalie na ulinzi wake, nisitende dhambi tena.
Baba yetu...
Salamu Maria...
Atukuzwe Baba...
K. Ee Bwana utuhurumie
W. Utuhurumie.
k. Roho za waamini wapate rehema kwa Mungu, wapumzike kwa amani.
W. Amina.
V
Kwa Simoni heri ya kweli
Mimi pia Yesu nisaidie
Kuchukua mzigo wa ukombozi
Kuteswa, kuteswa pamoja nawe.
KITUO CHA TANO
Simoni wa Kirene anamsaidia Yesu
- Ee Yesu tunakuabudu, tunakushukuru.
- Kwa kuwa umewakomboa watu kwa msalaba wako mtakatifu.
Nausifu ukarimu wa Simoni wa Kirene. Ee Bwana unijalie ukarimu kama huo, nitie ushujaa
kama huo, niitikie nami wito wa kukusaidia kuchukua msalaba.
Nitoe zaka na michango yote ya uenezaji wa dini. Nijitolee mimi mwenyewe katika kazi
ya maendeleo ya dini. Uwajalie vijana wengi wito wa Upadri, waweze kuchukua msalaba pamoja
nawe kwa ajili ya wokovu wa dunia. Uwaimarishe viongozi wa dini. Ustawishe moyoni mwa
waamini wote mwamko wa utume.
Baba yetu...
Salamu Maria...
Atukuzwe Baba...
K. Ee Bwana utuhurumie
W. Utuhurumie.
k. Roho za waamini wapate rehema kwa Mungu, wapumzike kwa amani.
W. Amina.
VI
Uso wa Yesu malaika
Bethlehemu walikuabudu
Bahati yake Veronika
Kupangusa, kupangusa mfalme wa mbingu.
KITUO CHA SITA
Veronika anapangusa uso wa Yesu
- Ee Yesu tunakuabudu, tunakushukuru.
- Kwa kuwa umewakomboa watu kwa msalaba wako mtakatifu.
Mama huyu ni kinyume kabisa cha Pilato. Veronika anajua analopaswa kutenda, na analitenda
bila kujali macho na maneno ya makundi ya watu waovu.
Ee Yesu uliyemtuza Veronika zawadi ya picha ya uso wako juu ya kitambaa, unijalie ushupavu
na ujasiri wake wa kutenda mema, ili roho yangu ipambwe kwa chapa ya uungwana na utakatifu
wako.
Baba yetu...
Salamu Maria...
Atukuzwe Baba...
K. Ee Bwana utuhurumie
W. Utuhurumie.
k. Roho za waamini wapate rehema kwa Mungu, wapumzike kwa amani.
W. Amina.
VII
Wakimvuta huku na huku
Wauaji wanamchokesha bure
Chini wamtupa bado kwa nguvu
Aibu, aibu yao milele.
KITUO CHA SABA
Yesu anaanguka mara ya pili
- Ee Yesu tunakuabudu, tunakushukuru.
- Kwa kuwa umewakomboa watu kwa msalaba wako mtakatifu.
Ee Yesu uliyelegea mno kwa mateso makali unapoanguka mara ya pili kwa ajili ya udhaifu wa
mwili wanionya kwamba hata mimi naweza kurudi dhambini kwa udhaifu wa moyo.
Nipe basi neema ya kuepuka nafasi za dhambi na visa vyenye kunikwaza na kunirudisha
dhambini
Baba yetu...
Salamu Maria...
Atukuzwe Baba...
K. Ee Bwana utuhurumie
W. Utuhurumie.
k. Roho za waamini wapate rehema kwa Mungu, wapumzike kwa amani.
W. Amina.
VIII
Wanawake wa Israeli
Musilie kwa sababu hiyo
Walilieni hao kwa dhambi zao
Upanga, upanga ni juu yao.
KITUO CHA NANE
Akina mama wanamlilia Yesu
- Ee Yesu tunakuabudu, tunakushukuru.
- Kwa kuwa umewakomboa watu kwa msalaba wako mtakatifu.
Asanteni sana akina mama kwa moyo wenu wa huruma.
Ee Yesu uliyetulizwa na wanawake, unipe moyo wa kuwaheshimu akina mama wote. Uwaite na
wasichana wengi waingie utawa, ili watulize Moyo wako mtakatifu kwa sala na sadaka zao.
Baba yetu...
Salamu Maria...
Atukuzwe Baba...
K. Ee Bwana utuhurumie
W. Utuhurumie.
k. Roho za waamini wapate rehema kwa Mungu, wapumzike kwa amani.
W. Amina.
IX
Mwokozi sasa ni ya tatu
Waanguka chini ya msalaba
Katika dhambi za ulegevu
Nijue, nijue kutubu hima.
KITUO CHA TISA
Yesu anaanguka mara ya tatu
- Ee Yesu tunakuabudu, tunakushukuru.
- Kwa kuwa umewakomboa watu kwa msalaba wako mtakatifu.
Ee Yesu unayezidi kudhoofika kwa mateso unaanguka mara ya tatu, upate kunistahilia neema
ya kuutiisha mwili wangu na kuusulubisha. Licha ya kuepuka nafasi za dhambi.
Mara nyingi mno ninajibovusha kwa kupenda mno starehe, anasa na tafrija. Ee Yesu mwema,
nisaidie kuufuata mfano wa Mtakatifu Paulo, niutese mwili wangu na kuutumikisha,
ili nipate siku moja tuzo mbinguni.
Baba yetu...
Salamu Maria...
Atukuzwe Baba...
K. Ee Bwana utuhurumie
W. Utuhurumie.
k. Roho za waamini wapate rehema kwa Mungu, wapumzike kwa amani.
W. Amina.
X
Mje malaika wa mbingu
Funikeni mwiliwe kwa huruma
Vidonda vyake na utupu
Askari, askari wamemvua.
KITUO CHA KUMI
Yesu anavuliwa nguo
- Ee Yesu tunakuabudu, tunakushukuru.
- Kwa kuwa umewakomboa watu kwa msalaba wako mtakatifu.
Askari wanamvua kwa nguvu nguo yake, iliyogandamana na madonda yake; wanayaamsha mara moja mateso
yote aliyoteswa tangu mwanzo.
Ee Yesu unayavumilia mateso makali haya, upate kunifundisha kuuvua kwa nguvu moyoni mwangu
urafiki mbaya, au kitu kingine chochote kile kinachoharibu urafiki wa Mungu, hata ikinipasa
kutoa sadaka kubwa.
Baba yetu...
Salamu Maria...
Atukuzwe Baba...
K. Ee Bwana utuhurumie
W. Utuhurumie.
k. Roho za waamini wapate rehema kwa Mungu, wapumzike kwa amani.
W. Amina.
XI
Hapo mkristo ushike moyo
Bwana wako alazwa msalabani
Mara miguu na mikono
Yafungwa, yafungwa kwa misumari.
KITUO CHA KUMI NA MOJA
Yesu anasulibiwa msalabani
- Ee Yesu tunakuabudu, tunakushukuru.
- Kwa kuwa umewakomboa watu kwa msalaba wako mtakatifu.
Ee Yesu uliyepigiliwa misumari msalabani, nakutolea akili na utashi wangu, vifungwe pamoja
na miguu yako, nipate kuwaza, kusema na kutenda siku zote yale tu yanayolingana na utukufu
wa msalaba wako mtakatifu.
Ee Yesu, mimi ni mfungwa wako. Nisaidie kuimarisha kifungo hicho kwa sala, Sakramenti na
fadhila za kikristo.
Baba yetu...
Salamu Maria...
Atukuzwe Baba...
K. Ee Bwana utuhurumie
W. Utuhurumie.
k. Roho za waamini wapate rehema kwa Mungu, wapumzike kwa amani.
W. Amina.
XII
Yesu mpenzi nakuabudu
Msalabani unapohangaika
Nchi yatetemeka kwa hofu
Na jua, na jua linafifia.
KITUO CHA KUMI NA MBILI
Yesu anakufa msalabani
- Ee Yesu tunakuabudu, tunakushukuru.
- Kwa kuwa umewakomboa watu kwa msalaba wako mtakatifu.
Ee Yesu uliyekufa msalabani kwa ajili ya dhambi zangu, unijalie nichukie dhambi, nisiishi
kamwe katika dhambi.
Nifahamu kwamba nilipobatizwa kwa jina lako, nilibatizwa katika mauti yako, ili utu wangu
wa kale usulibishwe nawe, mwili wa dhambi uangamizwe, nisitumikie tena dhambi.
Baba yetu...
Salamu Maria...
Atukuzwe Baba...
K. Ee Bwana utuhurumie
W. Utuhurumie.
k. Roho za waamini wapate rehema kwa Mungu, wapumzike kwa amani.
W. Amina.
XIII
Mama Maria mtakatifu
Upokee maiti ya mwanao
Tumemwua kwa dhambi zetu
Twatubu, twatubu kwake na kwako.
KITUO CHA KUMI NA TATU
Yesu anashushwa msalabani
- Ee Yesu tunakuabudu, tunakushukuru.
- Kwa kuwa umewakomboa watu kwa msalaba wako mtakatifu.
Ee Yesu uliyeshushwa msalabani baada ya kufa, unijalie nidumu katika maisha ya kujitoa
sadaka mpaka siku ya kufa kwangu.
Nielewe na nikubali kwamba baada tu ya kufa ndio mwisho wa vita na mashindano ya kikristo.
Baba yetu...
Salamu Maria...
Atukuzwe Baba...
K. Ee Bwana utuhurumie
W. Utuhurumie.
k. Roho za waamini wapate rehema kwa Mungu, wapumzike kwa amani.
W. Amina.
XIV
Pamoja nawe kaburini
Zika dhambi na ubaya wa moyo
Yesu tuwe wakristo kweli
Twakupa, twakupa sasa mapendo.
KITUO CHA KUMI NA NNE
Yesu anazikwa kaburini
- Ee Yesu tunakuabudu, tunakushukuru.
- Kwa kuwa umewakomboa watu kwa msalaba wako mtakatifu.
Ee Yesu, ulizikwa kaburini, ukafufuka siku ya tatu. Mimi pia nilizikwa pamoja nawe kwa njia
ya Ubatizo katika mauti yako.
Kwa vile wewe ulifufuka katika wafu kwa njia ya utukufu wa Baba, unijalie nami nifufuke,
yaani nishike mwenendo mpya, mwenendo wa uzima wa neema.
Baba yetu...
Salamu Maria...
Atukuzwe Baba...
K. Ee Bwana utuhurumie
W. Utuhurumie.
k. Roho za waamini wapate rehema kwa Mungu, wapumzike kwa amani.
W. Amina.
XV
Katika roho yangu Bwana
Chora mateso niliyo kutesa
Nisiyasahau madeni
Na kazi, na kazi ya kuokoka.
(Hiari yako - mbele ya altare)
KITUO CHA KUMI NA TANO
Yesu amefufuka
- Ee Yesu tunakuabudu, tunakushukuru.
- Kwa kuwa umewakomboa watu kwa msalaba wako mtakatifu.
Habari njema aliyotuletea Yesu ni kwamba baada ya kila Ijumaa Kuu huja sikukuu ya Pasaka;
kwamba punje ya ngano isipoanguka ikafa, hukaa hali hiyohiyo peke yake; bali ikifa, hutoa
mazao mengi.
Twakushukuru, ee Yesu, kwa mateso yako, lakini twakushukuru hasa kwa ufufuko wako, kwa
kuwa huo ndio unaotupa hakika ya kuwa hatukuzaliwa kwa ajili ya mateso na maumivu, bali
kwa ajili ya heri ya milele.
Baba yetu...
Salamu Maria...
Atukuzwe Baba...
K. Ee Bwana utuhurumie
W. Utuhurumie.
k. Roho za waamini wapate rehema kwa Mungu, wapumzike kwa amani.
W. Amina.
SALA YA MWISHO
Mbele ya Altare:
Yesu wangu, kwa uchungu wote ulioona juu ya msalaba, na kwa kuzimia kwako
kwa ukali wa mateso, unijalie nguvu ya kuvumilia kwa moyo taabu zote sasa na saa ya kuzimia
kwangu. Nawe Maria Mamangu, kwa uchungu wote ambao moyo wako umejaa ulipomwona mwanao mpenzi
kuinama kichwa na kuzimia, unifadhili nife kifo chema.
Kwa jina la Baba, na la Mwana, na la Roho Mtakatifu: Amina.