6

Wanawake
1 Ewe mwanamke uliye mzuri sana; amekwenda wapi huyo mpenzi wako? Ameelekea wapi mpenzi wako ili tupate kushirikiana nawe katika kumtafuta?

Bibi arusi
2 Mpenzi wangu amekwenda bustanini mwake, mahali ambapo rihani hustawi. Yeye analisha kondoo wake na kukusanya yungiyungi.
3 Mimi ni wake mpenzi wangu, naye ni wangu; yeye huwalisha kondoo wake penye yungiyungi.

Shairi la tano
Bwana arusi

4 Mpenzi wangu, wewe u mzuri kama Tirza, wapendeza kama Yerusalemu, unatisha kama jeshi lenye bendera.
5 Hebu tazama kando tafadhali; ukinitazama nahangaika. Nywele zako ni kama kundi la mbuzi, wateremkao chini ya milima ya Gileadi.
6 Meno yako kama kundi la kondoo majike wanaoteremka baada ya kuogeshwa. Kila mmoja amezaa mapacha, na hakuna yeyote aliyefiwa.
7 Mashavu yako ni kama nusu mbili za komamanga, nyuma ya shela lako.
8 Wapo malkia sitini, masuria themanini, na wasichana wasiohesabika!
9 Hua wangu, mzuri wangu, ni mmoja tu, na ni kipenzi cha mama yake; yeye ni wa pekee kwa mama yake. Wasichana humtazama na kumwita heri, nao malkia na masuria huziimba sifa zake.
10 Nani huyu atazamaye kama pambazuko? Mzuri kama mwezi, mwangavu kama jua, na anatisha kama jeshi lenye bendera.
11 Nimeingia katika bustani ya milozi kutazama machipuko ya bondeni, kuona kama mizabibu imechanua, na mikomamanga imechanua maua.
12 Bila kutazamia, mpenzi wangu, akanitia katika gari la mkuu.

Wanawake
13 Rudi, rudi ewe msichana wa Mshulami. Rudi, rudi tupate kukutazama.

Bibi arusi
Mbona mwataka kunitazama miye Mshulami kana kwamba mnatazama ngoma kati ya majeshi mawili?

Generic placeholder image