15
Mfano wa mzabibu 1 Neno la Mwenyezi-Mungu lilinijia: 2 “Wewe mtu! Je, mti wa mzabibu ni bora kuliko miti mingine msituni? 3 Je, mti wake wafaa kutengenezea kitu chochote? Je, watu huweza kutengeneza kigingi kutoka mti huo ili waweze kutundikia vitu? 4 Huo wafaa tu kuwashia moto. Tena moto unapoteketeza sehemu yake ya mwanzo na ya mwisho na kuikausha sehemu ya katikati, je, hiyo yafaa kwa kitu chochote? 5 Ulipokuwa haujachomwa ulikuwa haufai kitu, sembuse sasa baada ya kuteketezwa kwa moto na kuwa makaa! Haufai kitu kabisa. 6 Basi, mimi Bwana Mwenyezi-Mungu nasema hivi: Kama vile nilivyoutoa mti wa mzabibu kati ya miti ya msituni, ukateketezwa motoni, ndivyo nilivyotoa wakazi wa Yerusalemu. 7 Nitawakabili vikali. Hata kama wataukimbia moto, huo moto utawateketeza. Hapo nitakapowakabili vikali, ndipo mtakapotambua kuwa mimi ni Mwenyezi-Mungu. 8 Kwa kuwa wamekosa uaminifu kwangu, nitaifanya nchi yao kuwa ukiwa. Mimi Bwana Mwenyezi-Mungu nimesema.”