ALHAMISI JUMA 26 LA MWAKA WA 2
MASOMO
SOMO: Ayu.19:21-27
Ayubu alisema: Nihurumieni, nihurumieni, enyi rafiki zangu, Kwa maana mkono wa Mungu umenigusa.
Mbona ninyi mnaniudhi kama Mungu, Wala hamkutosheka na nyama yangu? Laiti maneno yangu yangeandikwa
sasa! Laiti yangeandikwa kitabuni! Yakachorwa katika mwamba milele, Kwa kalamu ya chuma na risasi.
Lakini mimi najua ya kuwa Mteteaji wangu yu hai, Na ya kuwa hatimaye atasimama juu ya nchi. Na baada
ya ngozi yangu kuharibiwa hivi, Lakini, pasipokuwa na mwili wangu nitamwona Mungu; Nami nitamwona
mimi nafsi yangu, Na macho yangu yatamtazama, wala si mwingine.
WIMBO WA KATIKATI: Zab.27:7-9,13-14(K)13
1. Ee Bwana, usikie, kwa sauti yangu ninalia,
Unifadhili, unijibu.
Uliposema, Nitafuteni uso wangu,
Moyo wangu umekuambia,
Bwana, uso wako nitautafuta.
(K) Naamini ya kuwa nitauona wema wa Bwana katika nchi ya walio hai.
2. Usinifiche uso wako,
Usijiepushe na mtumishi wako kwa hasira.
Umekuwa msaada wangu, usinitupe,
Wala usiniache, Ee Mungu wa wokovu wangu. (K)
3. Naamini ya kuwa nitauona wema wa Bwana
Katika nchi ya walio hai.
Umngoje Bwana, uwe hodari,
Upige moyo konde, naam, umngoje Bwana. (K)
SHANGILIO: Yn.8:12
Aleluya, aleluya!
Mimi ndimi nuru ya ulimwengu, asema Bwana, yeye anifuataye hatakwenda gizani kamwe,
bali atakuwa na nuru ya uzima.
Aleluya!
INJILI: Lk.10:1-12
Bwana aliweka wafuasi wengine, sabini na wawili, akawatuma wawili wawili wamtangulie kwenda
kila mji na kila mahali alipokusudia kwenda mwenyewe. Akawaambia, Mavuno ni mengi, lakini watenda
kazi ni wachache; basi mwombeni Bwana wa mavuno apeleke watenda kazi katika mavuno yake. Enendeni;
angalieni, nawatuma kama wana-kondoo kati ya mbwa-mwitu. Msichukue mfuko, wala mkoba, wala viatu;
wala msimwamkie mtu njiani. Na nyumba yoyote mtakayoingia, semeni kwanza, Amani iwemo nyumbani humu;
na akiwamo mwana wa amani, amani yenu itamkalia; la, hayumo, amani yenu itarudi kwenu. Basi, kaeni
katika nyumba iyo hiyo, mkila na kunywa vya kwao; maana, mtenda kazi amestahili kupewa ujira wake.
Msihame-hame kutoka nyumba hii kwenda nyumba hii. Na mji wowote mtakaouingia, wakiwakaribisha, vileni
vyakula viwekwavyo mbele yenu; wapozeni wagonjwa waliomo, waambieni, ufalme wa Mungu umewakaribia. Na
mji wowote mtakaouingia, nao hawawakaribishi, tokeni humo, nanyi mkipita katika njia zake semeni, Hata
mavumbi ya mji wenu yaliyogandamana na miguu yentu tunayakung’uta juu yenu. Lakini jueni hili, ya kuwa
Ufalme wa Mungu umekaribia. Nawaambia ya kwamba siku ile itakuwa rahisi zaidi Sodomo kuistahimili
adhabu yake kuliko mji huo.