13

Vita dhidi ya Wafilisti
1 Sauli alikuwa na umri wa miaka kadha wa kadha alipoanza kutawala. Na alitawala Israeli kwa muda wa miaka … miwili.
2 Sauli aliwachagua Waisraeli 3,000. Kati yao, 2,000 alikuwa nao huko Mikmashi na katika nchi ya milima ya Betheli. Elfu moja aliwaweka huko Gibea katika eneo la Benyamini. Hao aliwaweka chini ya mwanawe Yonathani. Watu wengine wote waliobakia, aliwarudisha, kila mtu nyumbani kwake.
3 Yonathani alishinda kambi ya kijeshi ya Wafilisti huko Geba, na Wafilisti wote walisikia juu ya habari hizo. Hivyo Sauli alipiga tarumbeta katika nchi yote akatangaza, akisema, “Waebrania na wasikie.”
4 Waisraeli wote waliposikia kuwa Sauli alikuwa ameishinda ngome ya kijeshi ya Wafilisti, na kwamba Wafilisti wanawachukia sana Waisraeli, waliitwa kwenda kuungana na Sauli huko Gilgali.
5 Wafilisti walikuwa na magari 30,000, askari 6,000 wapandafarasi na kikosi cha askari wa miguu wengi kama mchanga wa pwani; wote walipanda juu na kupiga kambi yao huko Mikmashi, mashariki ya Beth-aveni.
6 Waisraeli walipoona wako taabuni (maana walikuwa wanashambuliwa vikali), walianza kujificha. Wengine walijificha mapangoni, wengine mashimoni, wengine kwenye miamba, wengine kwenye makaburi na wengine kwenye visima.
7 Wengine walivuka mto Yordani mpaka katika nchi ya Gadi na nchi ya Gileadi. Lakini Sauli alikuwa bado huko Gilgali na watu wote walimfuata wakitetemeka.
8 Sauli alimngoja Samueli kwa muda wa siku saba, kama Samueli alivyosema. Lakini Samueli hakuja huko Gilgali na watu walianza kumwacha Sauli.
9 Basi, Sauli akawaambia watu, “Nileteeni sadaka yenu ya kuteketezwa na zile za amani.” Naye akatolea sadaka ya kuteketezwa.
10 Mara tu alipokuwa anamaliza kutoa sadaka ya kuteketezwa, Samueli aliwasili. Sauli akatoka nje kwenda kumlaki Samueli na kumsalimia.
11 Samueli akamwuliza, “Umefanya nini?” Sauli akamjibu, “Nilipoona watu wananiacha, na wewe hukuja, katika muda wa siku ulizosema, na tena nilipoona Wafilisti wamejipanga tayari kwa vita huko Mikmashi,
12 nikawaza kwamba Wafilisti watakuja kunishambulia huko Gilgali. Tena nilikuwa bado sijaomba fadhili za Mwenyezi-Mungu. Ndipo nilipolazimika kutolea mimi mwenyewe sadaka ya kuteketezwa.”
13 Samueli akamjibu Sauli, “Umefanya kipumbavu. Hukutii aliyokuamuru Mwenyezi-Mungu, Mungu wako. Kama ungetii, Mwenyezi-Mungu angeudumisha milele ufalme wako juu ya Israeli.
14 Lakini sasa ufalme wako hautadumu kwa kuwa amri aliyokuamuru Mwenyezi-Mungu hukuitii. Mwenyezi-Mungu amejitafutia mtu mwingine ambaye atamtii kwa moyo wote, na huyo ndiye ambaye amemteua kuwa mtawala juu ya watu wake.”
15 Samueli akaondoka kutoka Gilgali na kwenda huko Gibea katika nchi ya Benyamini. Sauli alipowahesabu watu waliokuwa pamoja naye, aliona wako watu 600 tu.
16 Sauli na Yonathani mwanawe pamoja na watu waliokuwa pamoja nao, walikaa huko Gibea katika nchi ya Benyamini na Wafilisti walipiga kambi huko Mikmashi.
17 Wafilisti walitoka kwenye kambi yao kwenda kuwashambulia wakiwa wako katika vikosi vitatu. Kikosi kimoja kilielekea Ofra katika nchi ya Shuali.
18 Kikosi kingine kilielekea Beth-horoni, na kikosi kingine kikageukia njia ielekeayo bonde la Seboimu, kuelekea jangwani.
19 Wakati huo hapakuwepo na mhunzi yeyote katika nchi nzima ya Israeli, kwani Wafilisti walikusudia kuwazuia Waebrania wasije wakajitengenezea mapanga au mikuki.
20 Kila Mwisraeli alilazimika kuwaendea Wafilisti kunoa wembe wa plau yake au sururu au shoka au mundu wa kuvunia.
21 Waisraeli walikuwa wanalipa fedha theluthi mbili za shekeli kunoa wembe wa plau na sururu. Na bei ya kunoa shoka au kupata mchokoo ilikuwa theluthi moja ya shekeli.
22 Kwa hiyo siku ya vita hakuna mtu miongoni mwa wote waliokuwa pamoja na Sauli na Yonathani aliyekuwa na upanga au mkuki isipokuwa Sauli na Yonathani mwanawe.
23 Wafilisti walipeleka kikosi cha askari kwenda kulinda njia ya Mikmashi.

Generic placeholder image