102
Sala katika taabu(Sala ya mtu aliye katika shida na ambaye anamwekea Mwenyezi-Mungu malalamiko yake) 1 Usikie sala yangu, ee Mwenyezi-Mungu, na kilio changu kikufikie. 2 Usijifiche mbali nami wakati wa taabu! Unitegee sikio lako, unijibu upesi wakati ninapokuomba! 3 Siku zangu zapita kama moshi; mifupa yangu yaungua kama katika tanuri. 4 Nimepondwa moyoni kama nyasi na kunyauka; sina hata hamu ya chakula. 5 Kutokana na kusononeka kwangu, nimebaki mifupa na ngozi. 6 Nimekuwa kama ndege wa jangwani; kama bundi kwenye mahame. 7 Ninalala macho wazi, kama ndege mkiwa juu ya paa. 8 Mchana kutwa maadui zangu wananisimanga, wanaonidhihaki hutumia jina langu kulaania. 9 Majivu yamekuwa chakula changu, machozi nayachanganya na kinywaji changu, 10 kwa sababu ya ghadhabu na hasira yako, maana umeniokota na kunitupilia mbali. 11 Maisha yangu ni kama kivuli cha jioni; ninanyauka kama nyasi. 12 Lakini wewe, ee Mwenyezi-Mungu, watawala milele; jina lako lakumbukwa vizazi vyote. 13 Wewe utainuka na kuurehemu mji wa Siyoni; maana wakati umefika wa kuutendea mema; wakati wake uliopangwa umefika. 14 Watumishi wako wanauthamini sana, ujapokuwa magofu sasa; wanauonea huruma, ingawa umeharibika kabisa. 15 Mataifa yataliheshimu jina la Mwenyezi-Mungu; wafalme wote duniani wataogopa utukufu wake. 16 Mwenyezi-Mungu ataijenga upya Siyoni, na kuonekana alivyo mtukufu. 17 Ataikubali sala ya fukara; wala hatayakataa maombi yao. 18 Andika jambo hili kwa ajili ya vizazi vijavyo; watakaozaliwa baadaye wamsifu Mwenyezi-Mungu. 19 Kwamba aliangalia chini kutoka patakatifu pake juu, Mwenyezi-Mungu aliangalia dunia kutoka mbinguni, 20 akasikia lalamiko la wafungwa; akawaachilia huru waliohukumiwa kuuawa. 21 Hivyo watu watatangaza jina la Mwenyezi-Mungu huko Siyoni; sifa zake zitatangazwa huko Yerusalemu, 22 wakati mataifa yatakapokusanyika pamoja na falme zitakutana kumwabudu Mwenyezi-Mungu. 23 Mungu amenipunguzia nguvu ningali kijana; ameyafupisha maisha yangu. 24 Ee Mungu wangu, usinichukue sasa wakati ningali bado kijana. Ee Mwenyezi-Mungu wewe wadumu milele. 25 Wewe uliiumba dunia zamani za kale, mbingu ni kazi ya mikono yako. 26 Hizo zitatoweka, lakini wewe wabaki; hizo zitachakaa kama vazi. Utazitupilia mbali kama nguo, nazo zitapotelea mbali. 27 Lakini wewe ni yuleyule daima, na maisha yako hayana mwisho. 28 Watoto wa watumishi wako watakaa salama; wazawa wao wataimarishwa mbele yako.