149
Wimbo wa ushindi 1 Msifuni Mwenyezi-Mungu! Mwimbieni Mwenyezi-Mungu wimbo mpya; msifuni katika kusanyiko la waaminifu! 2 Furahi ee Israeli kwa sababu ya Muumba wako, wakazi wa Siyoni shangilieni kwa sababu ya Mfalme wenu. 3 Lisifuni jina lake kwa ngoma, mwimbieni kwa ngoma na zeze. 4 Maana Mwenyezi-Mungu hupendezwa na watu wake; yeye huwapamba wanyonge kwa ushindi. 5 Watu waaminifu wafurahi kwa fahari; washangilie hata walalapo. 6 Wabubujike sifa kuu za Mungu, na panga zenye makali kuwili mikononi mwao, 7 wawalipe kisasi watu wa mataifa, wawaadhibu watu wasiomjua Mungu; 8 wawafunge wafalme wao kwa minyororo, na viongozi wao kwa pingu za chuma, 9 kusudi watekeleze adhabu iliyoamriwa! Hiyo ndiyo fahari ya waaminifu wa Mungu. Msifuni Mwenyezi-Mungu!