116
Shukrani kwa kuokolewa kifoni 1 Nampenda Mwenyezi-Mungu, kwa maana anisikia, maana amesikia kilio cha ombi langu. 2 Yeye amenitegea sikio, hivyo nitamwomba muda wote niishio. 3 Hatari ya kifo ilinizunguka, vitisho vya kaburi vilinivamia; nilijawa na mahangaiko na majonzi. 4 Kisha nikamlilia Mwenyezi-Mungu: “Ee Mwenyezi-Mungu, tafadhali unisalimishe!” 5 Mwenyezi-Mungu amejaa wema na uaminifu; Mungu wetu ni mwenye huruma. 6 Mwenyezi-Mungu huwalinda wanyofu; nilipokuwa nimekandamizwa aliniokoa. 7 Uwe na utulivu mkuu, ee nafsi yangu, maana Mwenyezi-Mungu amenitendea mema. 8 Ameniokoa kifoni na kufuta machozi yangu; akanilinda nisije nikaanguka. 9 Nitatembea mbele yake Mwenyezi-Mungu, katika nchi ya watu walio hai. 10 Nilikuwa na imani hata niliposema: “Mimi nimetaabika mno.” 11 Hata nilisema kwa hofu yangu: “Binadamu wote hawaaminiki!” 12 Nimrudishie nini Mwenyezi-Mungu, kwa ukarimu wote alionitendea? 13 Nitamtolea tambiko ya divai kwa kunikomboa, nitaomba kwa jina lake Mwenyezi-Mungu. 14 Nitamtimizia Mwenyezi-Mungu nadhiri zangu, mbele ya watu wake wote. 15 Kifo cha waaminifu wake Mwenyezi-Mungu si jambo dogo mbele yake. 16 Ee Mwenyezi-Mungu, mimi ni mtumishi wako; ni mtumishi wako, mtoto wa mjakazi wako; umenifungulia vifungo vyangu. 17 Nitakutolea tambiko za shukrani, na kukupa heshima zangu. 18 Nitakutimizia ahadi zangu, ee Mwenyezi-Mungu mbele ya watu wako wote, 19 waliokusanyika hekaluni mwako, katikati ya Yerusalemu. Msifuni Mwenyezi-Mungu!