115
Mungu mmoja wa kweli 1 Sio sisi, ee Mwenyezi-Mungu, sio sisi; bali wewe peke yako utukuzwe, kwa ajili ya fadhili zako na uaminifu wako. 2 Kwa nini mataifa yaseme: “Mungu wenu yuko wapi?” 3 Mungu wetu yuko mbinguni; yeye hufanya yote anayotaka. 4 Miungu yao ni ya fedha na dhahabu; imetengenezwa kwa mikono ya wanadamu. 5 Ina vinywa, lakini haisemi. Ina macho, lakini haioni. 6 Ina masikio, lakini haisikii. Ina pua, lakini hainusi. 7 Ina mikono, lakini haipapasi. Ina miguu, lakini haitembei. Haiwezi kamwe kutoa sauti. 8 Wote wanaoitengeneza wanafanana nayo, kadhalika na wote wanaoitumainia. 9 Enyi Waisraeli, mtumainieni Mwenyezi-Mungu; yeye ndiye msaada wenu na ngao yenu. 10 Enyi wazawa wa Aroni, mtumainieni Mwenyezi-Mungu; yeye ndiye msaada wenu na ngao yenu. 11 Enyi mnaomcha Mwenyezi-Mungu, mtumainini, yeye ndiye msaada wenu na ngao yenu. 12 Mwenyezi-Mungu atukumbuka na atatubariki; atawabariki watu wa Israeli, atawabariki wazawa wa Aroni. 13 Atawabariki wote wamchao, atawabariki wakubwa na wadogo. 14 Mwenyezi-Mungu awajalieni muongezeke; awajalieni muongezeke nyinyi na wazawa wenu! 15 Mbarikiwe na Mwenyezi-Mungu, aliyeziumba mbingu na dunia. 16 Mbingu ni mali yake Mwenyezi-Mungu, bali dunia amewapa binadamu. 17 Wafu hawamsifu Mwenyezi-Mungu, wala wale wanaoshuka katika nchi ya kimya. 18 Lakini sisi tulio hai twamsifu Mwenyezi-Mungu; tutamsifu sasa na hata milele. Msifuni Mwenyezi-Mungu!