92
Wimbo wa kumsifu Mungu(Zaburi. Wimbo wa siku ya Sabato) 1 Ni vema kukushukuru, ee Mwenyezi-Mungu, kuliimbia sifa jina lako, ee Mungu Mkuu. 2 Ni vema kutangaza fadhili zako asubuhi, na uaminifu wako nyakati za usiku, 3 kwa muziki wa zeze na kinubi, kwa sauti tamu ya zeze. 4 Ee Mwenyezi-Mungu, matendo yako yanifurahisha; nitashangilia kwa sababu ya mambo yote uliyotenda. 5 Matendo yako, ee Mwenyezi-Mungu, ni makuu mno! Mawazo yako ni mazito mno! 6 Mtu mpumbavu hawezi kufahamu, wala mjinga hajui jambo hili: 7 Kwamba waovu waweza kustawi kama nyasi, watenda maovu wote waweza kufanikiwa, lakini mwisho wao ni kuangamia milele, 8 bali wewe, ee Mwenyezi-Mungu, u mkuu milele. 9 Hao maadui zako, ee Mwenyezi-Mungu, naam, hao maadui zako, hakika wataangamia; wote watendao maovu, watatawanyika! 10 Wewe umenipa nguvu kama nyati; umenimiminia mafuta ya kuburudisha. 11 Kwa macho nimeona maadui zangu wameshindwa; nimesikia kilio chao watendao maovu. 12 Waadilifu hustawi kama mitende; hukua kama mierezi ya Lebanoni! 13 Kama miti iliyopandwa nyumbani mwa Mwenyezi-Mungu, hustawi katika nyua za Mungu wetu; 14 huendelea kuzaa matunda hata uzeeni; daima wamejaa utomvu na wabichi; 15 wapate kutangaza kwamba Mwenyezi-Mungu ni mnyofu, Mwamba wangu, kwake hamna upotovu.