118
Sala ya shukrani 1 Mshukuruni Mwenyezi-Mungu, kwa kuwa ni mwema, kwa maana fadhili zake zadumu milele. 2 Watu wa Israeli na waseme: “Fadhili zake zadumu milele.” 3 Wazawa wa Aroni na waseme: “Fadhili zake zadumu milele.” 4 Wote wamchao Mwenyezi-Mungu na waseme: “Fadhili zake zadumu milele.” 5 Katika taabu yangu nilimwomba Mwenyezi-Mungu, naye akanisikia na kuniweka huru. 6 Mwenyezi-Mungu yuko nami, siogopi kitu; binadamu ataweza kunifanya nini? 7 Mwenyezi-Mungu yuko nami, kunisaidia; nami nitawaona maadui zangu wameshindwa. 8 Afadhali kukimbilia usalama kwa Mwenyezi-Mungu, kuliko kumtumainia mwanadamu. 9 Afadhali kukimbilia usalama kwa Mwenyezi-Mungu, kuliko kuwatumainia viongozi wa dunia. 10 Mataifa yote yalinizingira, lakini kwa jina la Mwenyezi-Mungu nikayaangamiza! 11 Yalinizunguka kila upande, lakini kwa jina la Mwenyezi-Mungu, nikayaangamiza! 12 Yalinizunguka, mengi kama nyuki, lakini yakateketea kama kichaka motoni; kwa jina la Mwenyezi-Mungu niliyaangamiza! 13 Nilishambuliwa mno karibu nishindwe, lakini Mwenyezi-Mungu alinisaidia. 14 Mwenyezi-Mungu ni nguvu yangu kuu; yeye mwenyewe ndiye wokovu wangu. 15 Sauti za furaha ya ushindi zasikika hemani mwao waadilifu: “Mkono wa Mwenyezi-Mungu umetenda mambo makuu! 16 Mkono wa nguvu wa Mwenyezi-Mungu umeleta ushindi! Mkono wa Mwenyezi-Mungu umetenda mambo makuu!” 17 Sitakufa, bali nitaishi, na kusimulia matendo ya Mwenyezi-Mungu. 18 Mwenyezi-Mungu ameniadhibu sana, lakini hakuniacha nife. 19 Nifungulie milango ya watu waadilifu, niingie na kumshukuru Mwenyezi-Mungu! 20 Huu ndio mlango wa Mwenyezi-Mungu, watu waadilifu watapitia humo. 21 Nakushukuru, ee Mungu kwa kunijibu; kwa sababu wewe ni wokovu wangu. 22 Jiwe walilokataa waashi, limekuwa jiwe kuu la msingi. 23 Hiyo ni kazi yake Mwenyezi-Mungu nayo ni ya ajabu sana kwetu. 24 Hii ndiyo siku aliyoifanya Mwenyezi-Mungu; tushangilie na kufurahi. 25 Tafadhali utuokoe, ee Mwenyezi-Mungu! Tafadhali utufanikishe, ee Mwenyezi-Mungu! 26 Abarikiwe huyo ajaye kwa jina la Mwenyezi-Mungu! Twawabariki kutoka nyumbani mwa Mwenyezi-Mungu 27 Mwenyezi-Mungu ni Mungu; yeye ametujalia mwanga wake Shikeni matawi ya sherehe, mkiandamana mpaka madhabahuni. 28 Wewe ni Mungu wangu, nami ninakushukuru; ninakutukuza, ee Mungu wangu. 29 Mshukuruni Mwenyezi-Mungu kwa kuwa ni mwema, kwa maana fadhili zake zadumu milele.