76
Mungu mshindi(Kwa Mwimbishaji: Na ala za nyuzi za muziki. Zaburi ya Asafu. Wimbo) 1 Mungu anajulikana katika Yuda; jina lake ni kuu katika Israeli. 2 Makao yake yamo huko Salemu; maskani yake huko Siyoni. 3 Huko alivunja mishale ya adui; alivunja ngao, panga na silaha za vita. 4 Wewe, ee Mungu, watukuka mno; umejaa fahari kuliko milima ya milele. 5 Wenye nguvu walipokonywa nyara zao, sasa wamelala usingizi wa kifo, mashujaa wa vita hawakuweza kutumia mikono yao. 6 Ulipowakemea, ee Mungu wa Yakobo, farasi na wapandafarasi walikufa ganzi. 7 Wewe, ee Mungu, ni wa kutisha mno! Nani awezaye kustahimili mbele yako ukikasirika? 8 Ulijulisha hukumu yako toka mbinguni; dunia iliogopa na kunyamaza; 9 wakati ulipoinuka kutekeleza hukumu, kuwaokoa wote wanaodhulumiwa duniani. 10 Ghadhabu ya watu husababisha tu sifa kwako; na waliookoka vitani watafanya sikukuu zako. 11 Mtimizieni Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu ahadi zenu; enyi mlio karibu mpeni zawadi Mungu wa kutisha. 12 Yeye huzitoa roho za wakuu; huwatisha wafalme wa dunia.