63
Hamu ya kuwa pamoja na Mungu(Zaburi ya Daudi wakati alipokuwa katika jangwa la Yudea) 1 Ee Mungu, wewe u Mungu wangu, nami nakutafuta kwa moyo; roho yangu inakutamani kama mtu mwenye kiu; nina kiu kama nchi kavu isiyo na maji. 2 Nimetaka kukuona patakatifuni pako, niione nguvu yako na utukufu wako. 3 Fadhili zako ni bora kuliko maisha, nami nitakusifu kwa mdomo wangu. 4 Nitakushukuru maisha yangu yote; nitainua mikono yangu na kukuomba. 5 Roho yangu inafurahi kama kwa karamu na vinono; kwa shangwe nitaimba sifa zako. 6 Niwapo kitandani ninakukumbuka, usiku kucha ninakufikiria; 7 maana wewe umenisaidia daima. Kivulini mwa mabawa yako nitashangilia. 8 Roho yangu inaambatana nawe kabisa, mkono wako wa kulia wanitegemeza. 9 Lakini hao wanaotaka kuyaangamiza maisha yangu, watatumbukia chini kwenye makao ya wafu. 10 Watauawa kwa upanga, watakuwa chakula cha mbweha. 11 Lakini mfalme atafurahi kwa sababu ya Mungu; wanaoahidi kwa jina la Mungu watamsifu, lakini vinywa vya waongo vitafumbwa.