43
Sala ya mkimbizi yaendelea(Zaburi ya 42 yaendelea) 1 Onesha kuwa sina hatia ee Mungu; utetee kisa changu dhidi ya watu wabaya; uniokoe na watu waongo na waovu. 2 Nakimbilia usalama kwako ee Mungu; kwa nini umenitupilia mbali? Yanini niende huko na huko nikiomboleza kwa kudhulumiwa na adui yangu? 3 Upeleke mwanga na ukweli wako viniongoze, vinipeleke kwenye mlima wako mtakatifu, kwenye makao yako. 4 Hapo, ee Mungu, nitakwenda madhabahuni pako; nitakuja kwako, ee Mungu, furaha yangu kuu. Nitakusifu kwa zeze, ee Mungu, Mungu wangu. 5 Mbona ninahuzunika hivyo moyoni? Kwa nini nahangaika hivyo ndani mwangu? Nitamtumainia Mungu, nitamsifu tena yeye aliye msaada wangu na Mungu wangu.