58
Mungu hakimu wa mahakimu(Kwa Mwimbishaji: Mtindo “Usiharibu”. Utenzi wa Daudi) 1 Enyi watawala, je, mwahukumu kwa haki kweli? Je, mnawahukumu watu kwa adili? 2 La! Nyinyi mwafikiria tu kutenda maovu; nyinyi wenyewe mwaeneza dhuluma nchini. 3 Waovu wamepotoka tangu kuzaliwa kwao, waongo hao, wamekosa tangu walipozaliwa. 4 Wana sumu kama sumu ya nyoka; viziwi kama joka lizibalo masikio, 5 ambalo halisikii hata sauti ya mlozi, au utenzi wa mganga stadi wa uchawi. 6 Ee Mungu, wavunje meno yao, yangoe, ee Mwenyezi-Mungu, meno ya simba hao. 7 Watoweke kama maji yanayodidimia mchangani, kama nyasi wakanyagwe na kunyauka, 8 watoweke kama konokono ayeyukavyo, kama mimba iliyoharibika isiyoona kamwe jua! 9 Kabla hawajatambua, wangolewe kama miiba, michongoma au magugu. Kwa hasira ya Mungu, wapeperushwe mbali, wakiwa bado hai. 10 Waadilifu watafurahi waonapo waovu wanaadhibiwa; watatembea katika damu ya watu wabaya. 11 Watu wote watasema: “Naam, waadilifu hupata tuzo! Hakika yuko Mungu anayeihukumu dunia!”