148
Ulimwengu wote umsifu Mungu 1 Msifuni Mwenyezi-Mungu! Msifuni Mwenyezi-Mungu kutoka mbinguni, msifuni kutoka huko juu mbinguni. 2 Msifuni, enyi malaika wake wote, msifuni, enyi majeshi yake yote. 3 Msifuni, enyi jua na mwezi, msifuni, enyi nyota zote zingaazo. 4 Msifuni, enyi mbingu za juu, na maji yaliyo juu ya mbingu. 5 Vyote vilisifu jina la Mwenyezi-Mungu, maana yeye aliamuru, na vyote vikawa. 6 Yeye aliviweka mahali pao daima, kwa amri ambayo haiwezi kubatilishwa. 7 Msifuni Mwenyezi-Mungu kutoka duniani; enyi majoka ya baharini na vilindini, msifuni. 8 Msifuni enyi moto, mvua ya mawe na theluji, upepo wa tufani unaotimiza amri yake! 9 Msifuni enyi milima na vilima, miti ya matunda na misitu! 10 Msifuni enyi wanyama wa porini na wafugwao, viumbe vitambaavyo na ndege wote! 11 Msifuni enyi wafalme na mataifa yote; viongozi na watawala wote duniani! 12 Msifuni enyi wavulana na wasichana; wazee wote na watoto pia! 13 Nyote lisifuni jina la Mwenyezi-Mungu, maana jina lake peke yake latukuka; utukufu wake wapita dunia na mbingu. 14 Amewapa watu wake nguvu; heshima kwa watu wote waaminifu, watu wa Israeli wapenzi wake. Msifuni Mwenyezi-Mungu!