11
Kumtumainia Mungu(Kwa Mwimbishaji. Zaburi ya Daudi) 1 Kwake Mwenyezi-Mungu nakimbilia usalama; mnawezaje basi kuniambia: “Ruka kama ndege, mpaka milimani, 2 maana waovu wanavuta pinde; wameweka mishale tayari juu ya uta, wawapige mshale watu wema gizani! 3 Kama misingi ikiharibiwa, mtu mwadilifu atafanya nini?” 4 Mwenyezi-Mungu yumo katika hekalu lake takatifu; kiti cha enzi cha Mwenyezi-Mungu kiko mbinguni. Kwa macho yake huwachungulia wanadamu, na kujua kila kitu wanachofanya. 5 Mwenyezi-Mungu huwapima waadilifu na waovu; huwachukia kabisa watu wakatili. 6 Atawanyeshea waovu makaa ya moto na madini ya kiberiti; upepo wa hari utakuwa ndio adhabu yao. 7 Mwenyezi-Mungu ni mwadilifu na apenda uadilifu; watu wanyofu watakaa pamoja naye.