130
Kuomba msaada(Wimbo wa Kwenda Juu) 1 Toka upeo wa unyonge wangu, nakulilia, ee Mwenyezi-Mungu. 2 Ee Bwana, sikia sauti yangu, uitegee sikio sauti ya ombi langu. 3 Kama, ee Mwenyezi-Mungu ungekumbuka maovu yetu nani, ee Bwana, angeweza kusalimika? 4 Lakini kwako twapata msamaha, ili sisi tukuheshimu. 5 Namtumainia Mwenyezi-Mungu kwa moyo wangu wote; nina imani sana na neno lake. 6 Ninamtumainia Mwenyezi-Mungu kuliko walinzi wanavyongojea pambazuko; kuliko walinzi wanavyongojea kuche asubuhi. 7 Ee Israeli, umtumainie Mwenyezi-Mungu, maana kwake Mwenyezi-Mungu kuna fadhili, kwake kuna nguvu kubwa ya kutukomboa. 8 Yeye atawakomboa watu wa Israeli kutoka katika maovu yao yote.