6
Sala wakati wa taabu(Kwa Mwimbishaji: Na ala za nyuzi za muziki. Mtindo wa Sheminithi. Zaburi ya Daudi) 1 Ee Mwenyezi-Mungu, usinikemee kwa hasira yako; usiniadhibu kwa ghadhabu yako. 2 Unihurumie, ee Mwenyezi-Mungu, nimeishiwa nguvu; uniponye, ee Mwenyezi-Mungu, nataabika mpaka mifupani. 3 Ninahangaika sana rohoni mwangu. Ee Mwenyezi-Mungu, utakawia mpaka lini? 4 Unigeukie, ee Mwenyezi-Mungu, uniokoe; unisalimishe kwa sababu ya fadhili zako. 5 Huko kwa wafu hakuna anayekukumbuka; huko kuzimu ni nani awezaye kukusifu? 6 Niko hoi kwa kilio cha uchungu; kila usiku nalowesha kitanda changu kwa machozi; kwa kulia kwangu naulowesha mto wangu. 7 Macho yangu yamechoka kwa huzuni; yamefifia kwa kutaabishwa na adui. 8 Ondokeni kwangu enyi nyote watenda maovu! Maana Mwenyezi-Mungu amesikia kilio changu. 9 Mwenyezi-Mungu amesikia ombi langu; Mwenyezi-Mungu amekubali sala yangu. 10 Maadui zangu wote wataaibika na kufadhaika; watarudi nyuma na kuaibishwa ghafla.