25
Kumwomba Mungu uongozi na ulinzi(Zaburi ya Daudi) 1 Ee Mwenyezi-Mungu, kwako naielekeza nafsi yangu! 2 Nakutumainia wewe, ee Mungu wangu, usiniache niaibike; adui zangu wasifurahie kushindwa kwangu. 3 Usimwache anayekutumainia apate aibu; lakini waaibike wote wanaokuasi kwa makusudi. 4 Unijulishe njia zako, ee Mwenyezi-Mungu; unifundishe nifuate unayotaka. 5 Uniongoze katika ukweli wako na kunifundisha, kwani wewe ni Mungu, mwokozi wangu; ninakutegemea wewe kila siku. 6 Uikumbuke huruma yako ee Mwenyezi-Mungu; uzikumbuke na fadhili zako kuu, ambazo zimekuwako tangu kale. 7 Usikumbuke dhambi na makosa ya ujana wangu; unikumbuke kadiri ya fadhili zako, kwa ajili ya wema wako, ee Mwenyezi-Mungu. 8 Mwenyezi-Mungu ni mwema na mnyofu, kwa hiyo huwafundisha wenye dhambi njia. 9 Huwaongoza wanyenyekevu katika uadilifu; naam, huwafundisha hao njia yake. 10 Mwenyezi-Mungu hutenda kwa fadhili na uaminifu, kwa wale wanaoshika agano lake na maamuzi yake. 11 Kwa ajili ya jina lako, ee Mwenyezi-Mungu, unisamehe kosa langu kwani ni kubwa. 12 Kila mtu anayemcha Mwenyezi-Mungu, Mwenyezi-Mungu atamfunza njia ya kufuata. 13 Mtu wa namna hiyo atafanikiwa daima, na wazawa wake watamiliki nchi. 14 Mwenyezi-Mungu ni rafiki ya wale wamchao; yeye huwajulisha hao agano lake. 15 Namwangalia Mwenyezi-Mungu daima; yeye atainasua miguu yangu mtegoni. 16 Unielekee, ee Mungu, unionee huruma, maana mimi ni mpweke na mnyonge. 17 Uniondolee mahangaiko ya moyoni mwangu; unitoe katika mashaka yangu. 18 Uangalie mateso yangu na dhiki yangu; unisamehe dhambi zangu zote. 19 Angalia jinsi walivyo wengi maadui zangu; ona jinsi wanavyonichukia kwa ukatili. 20 Uyalinde maisha yangu, uniokoe; nakimbilia usalama kwako, usikubali niaibike. 21 Wema na uadilifu vinihifadhi, maana ninakutumainia wewe. 22 Ee Mungu, uwaokoe watu wako, Israeli; uwaokoe katika taabu zao zote.