26
Sala ya mtu mwema(Zaburi ya Daudi) 1 Ee Mwenyezi-Mungu, unitetee, maana nimeishi bila hatia, nimekutumainia wewe bila kusita. 2 Unijaribu, ee Mwenyezi-Mungu, na kunipima; uchunguze moyo wangu na akili zangu. 3 Fadhili zako ziko mbele ya macho yangu, ninaishi kutokana na uaminifu wako. 4 Sijumuiki na watu wapotovu; sishirikiani na watu wanafiki. 5 Nachukia mikutano ya wabaya; wala sitajumuika na waovu. 6 Nanawa mikono yangu kuonesha sina hatia, na kuizunguka madhabahu yako, ee Mwenyezi-Mungu, 7 nikiimba wimbo wa shukrani, na kusimulia matendo yako yote ya ajabu. 8 Ee Mwenyezi-Mungu, napenda makao yako, mahali unapokaa utukufu wako. 9 Usiniangamize pamoja na wenye dhambi, wala usinitupe pamoja na wauaji, 10 watu ambao matendo yao ni maovu daima, watu ambao wamejaa rushwa. 11 Lakini mimi ninaishi kwa unyofu; unihurumie na kunikomboa. 12 Mimi nimesimama mahali palipo imara; nitamsifu Mwenyezi-Mungu katika kusanyiko kubwa.