KITABU CHA PILI
(Zaburi 42–72)

42

Sala ya Mkimbizi
(Kwa Mwimbishaji. Utenzi wa Wakorahi)
1 Kama paa atamanivyo maji ya kijito, ndivyo ninavyokutamani, ee Mungu wangu!
2 Naona kiu ya Mungu, kiu ya Mungu aliye hai. Nitafika lini kwake na kuuona uso wake?
3 Machozi yamekuwa chakula changu mchana na usiku, waliponiambia kila siku: “Yuko wapi Mungu Wako!”
4 Nakumbuka tena mambo haya kwa majonzi moyoni mwangu: Jinsi nilivyokwenda na umati wa watu, nikawaongoza kwenda nyumbani kwa Mungu wakipiga vigelegele vya shukrani; umati wa watu wakifanya sherehe!
5 Mbona nasononeka hivyo moyoni? Kwa nini nahangaika hivyo ndani mwangu? Nitamtumainia Mungu, maana nitamsifu tena yeye aliye msaada wangu na Mungu wangu.
6 Nimesongwa na huzuni moyoni mwangu, kwa hiyo ninakukumbuka wewe, ee Mungu, kutoka katika eneo la Yordani, kutoka mlima Hermoni na Mizari.
7 Nimeporomoshewa mafuriko ya maji mafuriko ya maji yaja karibu nayo yaita maporomoko mapya. Mawimbi na mapigo yako yamenikumba.
8 Mwenyezi-Mungu atanijalia fadhili zake mchana; nami nimwimbie wimbo wa sifa usiku, nimwombe Mungu anipaye uhai.
9 Namwambia Mungu, mwamba wangu: “Kwa nini umenisahau? Yanini niende huko na huko nikiomboleza kwa kudhulumiwa na adui yangu?”
10 Nimepondwa kwa matukano yao, wanaponiuliza kila siku: “Yuko wapi, Mungu wako!”
11 Mbona nasononeka hivyo moyoni? Kwa nini nahangaika hivyo? Nitamtumainia Mungu, maana nitamsifu tena Mungu, aliye msaada wangu na Mungu wangu.

Generic placeholder image