34
Sifa kwa wema wa Mungu(Zaburi ya Daudi alipojifanya mwendawazimu mbele ya Abimeleki) 1 Nitamtukuza Mwenyezi-Mungu nyakati zote, sitaacha kamwe kuzitamka sifa zake. 2 Mimi nitaona fahari juu ya Mwenyezi-Mungu, wanyonge wasikie na kufurahi. 3 Mtukuzeni Mwenyezi-Mungu pamoja nami, sote pamoja tulisifu jina lake. 4 Nilimwomba Mwenyezi-Mungu naye akanijibu, na kuniondoa katika hofu zangu zote. 5 Mgeukieni Mungu mpate kufurahi; nanyi hamtaaibishwa kamwe. 6 Maskini alimlilia Mwenyezi-Mungu, naye akamsikia, na kumwokoa katika taabu zake zote. 7 Malaika wa Mwenyezi-Mungu huwalinda wote wamchao, na kuwaokoa katika hatari. 8 Jaribuni mwone Mwenyezi-Mungu alivyo mwema. Heri mtu anayekimbilia usalama kwake. 9 Mcheni Mwenyezi-Mungu enyi watakatifu wake; maana wenye kumcha hawatindikiwi na kitu. 10 Hata wanasimba hutindikiwa na kuona njaa; lakini wanaomtafuta Mwenyezi-Mungu hawakosi chochote chema. 11 Njoni enyi vijana mkanisikilize, nami nitawafundisha kumcha Mwenyezi-Mungu. 12 Je, watamani kufurahia maisha, kuishi maisha marefu na kufurahia mema? 13 Basi, acha kusema mabaya, na kuepa kusema uongo. 14 Jiepushe na uovu, utende mema; utafute amani na kuizingatia. 15 Mwenyezi-Mungu huwaangalia waadilifu, na kusikiliza malalamiko yao; 16 lakini huwapinga watu watendao maovu, awafutilie mbali kutoka duniani. 17 Waadilifu wakimlilia Mwenyezi-Mungu yeye huwasikia, na kuwaokoa katika taabu zao zote. 18 Mwenyezi-Mungu yu karibu na waliokufa moyo; huwaokoa wote waliokata tamaa kabisa. 19 Mateso ya mwadilifu ni mengi, lakini Mwenyezi-Mungu humwokoa kutoka yote. 20 Huvilinda viungo vya mwili wake wote, hakuna hata mfupa wake mmoja utakaovunjwa. 21 Ubaya huwaletea waovu kifo; wanaowachukia waadilifu wataadhibiwa. 22 Mwenyezi-Mungu huokoa maisha ya watumishi wake, wote wanaomkimbilia hawataadhibiwa.