80
Maombi kwa ajili ya taifa(Kwa Mwimbishaji: Mtindo wa Yungiyungi. Zaburi ya Asafu) 1 Utege sikio, ewe Mchungaji wa Israeli, uwaongozaye wazawa wa Yosefu kama kondoo. Ewe ukaaye juu ya viumbe vyenye mabawa, uangaze, 2 mbele ya Efraimu, Benyamini na Manase. Uoneshe nguvu yako, uje kutuokoa! 3 Uturekebishe, ee Mungu; utuangalie kwa wema, nasi tutaokoka. 4 Ee Mwenyezi-Mungu, Mungu wa majeshi, hata lini utazikasirikia sala za watu wako? 5 Umefanya huzuni iwe chakula chetu; umetunywesha machozi kwa wingi. 6 Umetufanya tuwe dharau kwa jirani zetu; maadui zetu wanatudhihaki. 7 Ee Mungu wa majeshi, uturekebishe, utuangalie kwa wema, nasi tutaokoka. 8 Ulileta mzabibu kutoka Misri; ukawafukuza watu wa mataifa mengine, na kuupanda katika nchi yao. 9 Uliupalilia upate kukua, nao ukatoa mizizi na kuenea kote nchini. 10 Uliifunika milima kwa kivuli chake, na matawi yake yakawa kama mierezi mikubwa. 11 Matawi yake yalienea mpaka baharini; machipukizi yake mpaka kando ya mto Eufrate. 12 Mbona ulibomoa kuta zilizouzunguka? Sasa kila apitaye anachuma zabibu zake; 13 nguruwe mwitu wanauharibu, na wanyama wa porini wanautafuna! 14 Utugeukie tena ee Mungu wa majeshi. Uangalie toka mbinguni, uone; ukautunze mzabibu huo. 15 Uulinde mche ulioupanda kwa mkono wako; hilo chipukizi uliloimarisha wewe mwenyewe. 16 Watu walioukata na kuuteketeza, uwatazame kwa ukali, waangamie. 17 Mkono wako umkinge huyo uliyemfadhili; huyo uliyemteua kwa ajili yako. 18 Hatutakuacha na kukuasi tena; utujalie uhai, nasi tutakusifu. 19 Ee Mwenyezi-Mungu wa majeshi uturekebishe; utuangalie kwa wema, nasi tutaokoka.