2
Mfalme mteule wa Mungu 1 Kwa nini mataifa yanafanya ghasia? Mbona watu wanafanya njama za bure? 2 Wafalme wa dunia wanajitayarisha; watawala wanashauriana pamoja, dhidi ya Mwenyezi-Mungu na mteule wake. 3 Wanasema: “Tujiondoe katika utawala wao; tutupilie mbali minyororo yao!” 4 Mwenyezi-Mungu atawalaye juu mbinguni, anawacheka na kuwadhihaki. 5 Kisha, anawakaripia kwa ghadhabu, na kuwatisha kwa hasira, akisema: 6 “Nimemtawaza mfalme niliyemteua, anatawala Siyoni, mlima wangu mtakatifu!” 7 Mfalme asema: “Nitatangaza azimio la Mwenyezi-Mungu. Mungu aliniambia: ‘Wewe ni mwanangu, mimi leo nimekuwa baba yako. 8 Niombe nami nitakupa mataifa yawe urithi wako, na dunia nzima kuwa mali yako. 9 Utawaponda kwa fimbo ya chuma; utawavunja kama chungu cha mfinyanzi!’” 10 Sasa enyi wafalme, tumieni busara; sikilizeni onyo hili, enyi watawala wa dunia. 11 Mtumikieni Mwenyezi-Mungu kwa uchaji; 12 msujudieni na kutetemeka; asije akakasirika, mkaangamia ghafla; kwani hasira yake huwaka haraka. Heri yao wote wanaokimbilia usalama kwake!