38
Sala katika mateso(Zaburi ya Daudi ya matoleo) 1 Ee Mwenyezi-Mungu, usinikemee kwa hasira yako; usiniadhibu kwa ghadhabu yako. 2 Mishale yako imenichoma; mkono wako umenigandamiza. 3 Hamna mahali nafuu mwilini mwangu, kwa sababu umenikasirikia; hamna penye afya hata mifupani mwangu, kwa sababu ya dhambi yangu. 4 Nimefunikwa kabisa na dhambi zangu, zinanilemea kama mzigo mzito mno kwangu. 5 Madonda yangu yameoza na kunuka, na hayo ni matokeo ya ujinga wangu. 6 Nimepindika mpaka chini na kupondeka; mchana kutwa nazunguka nikiomboleza. 7 Viungo vyangu vimeshambuliwa na homa; mwilini mwangu hamna nafuu yoyote. 8 Nimelegea na kupondekapondeka; nasononeka kwa kusongwa moyoni. 9 Ee Bwana, wewe wajua tazamio langu lote; kwako hakikufichika kilio changu. 10 Moyo wanidunda, nguvu zimeniishia; hata macho yangu nayo yamekwisha fifia. 11 Rafiki na wenzangu wanaepa kuona mateso yangu, na jamaa zangu wanakaa mbali nami. 12 Wanaotaka kuniua wanatega mitego yao; wanaonitakia niumie wanatishia kuniangamiza. Mchana kutwa wanafanya mipango dhidi yangu. 13 Lakini mimi nimekuwa kama kiziwi, sisikii; nimekuwa kama bubu asiyeweza kusema kitu. 14 Naam, nimekuwa kama mtu asiyesikia, kama mtu asiye na chochote cha kujitetea. 15 Lakini ninakutumainia wewe, ee Mwenyezi-Mungu; wewe, ee Mwenyezi-Mungu, Mungu wangu, ndiwe utakayenijibu. 16 Nakuomba tu maadui wasinisimange, wasione fahari juu ya kuanguka kwangu. 17 Karibu sana nitaanguka; nakabiliwa na maumivu ya daima. 18 Naungama uovu wangu; dhambi zangu zanisikitisha. 19 Maadui zangu hawajambo, wana nguvu; ni wengi mno hao wanaonichukia bure. 20 Hao wanaonilipa maovu kwa wema wangu, wananipinga kwa sababu natenda mema. 21 Usinitupe, ee Mwenyezi-Mungu; ee Mungu wangu, usikae mbali nami. 22 Uje haraka kunisaidia; ewe Mwenyezi-Mungu, uliye wokovu wangu.