112
Furaha ya mtu mwema 1 Msifuni Mwenyezi-Mungu! Heri mtu anayemcha Mwenyezi-Mungu, anayefurahia sana kutii amri zake. 2 Wazawa wake watakuwa wenye nguvu nchini; watoto wa wanyofu watapata baraka. 3 Nyumbani kwake kutakuwa na mali nyingi; uadilifu wake wadumu milele. 4 Mtu mwema huangaziwa mwanga gizani; mtu mwenye huruma, mpole na mwadilifu. 5 Mtu mkarimu akopeshaye bila faida, hufanikiwa; mtu afanyaye shughuli zake kwa kutumia haki. 6 Mwadilifu hatashindwa kamwe, huyo atakumbukwa milele. 7 Hana haja ya kuogopa akipata habari mbaya; ana moyo thabiti na humtegemea Mwenyezi-Mungu. 8 Yuko imara moyoni, wala hataogopa; naye atawaona maadui zake wanashindwa. 9 Hutoa kwa ukarimu, huwapa maskini; uadilifu wake wadumu milele. Nguvu yake inatukuzwa kwa heshima. 10 Watu waovu huona hayo na kuudhika; husaga meno kwa chuki na kutoweka, matazamio ya mtu mbaya huishia patupu.