140
Sala ya kuomba ulinzi wa Mungu(Kwa Mwimbishaji. Zaburi ya Daudi) 1 Ee Mwenyezi-Mungu, uniokoe na watu wabaya, unikinge na watu wakatili. 2 Watu hao huwaza mabaya daima, huzusha magomvi kila mara. 3 Ndimi zao hatari kama za nyoka; midomoni mwao mna maneno ya sumu kama ya joka. 4 Ee Mwenyezi-Mungu, unilinde na makucha ya wabaya; unikinge na watu wakatili ambao wamepanga kuniangusha. 5 Wenye kiburi wamenitegea mitego, wametandaza kamba kama wavu, wameficha mitego njiani wanikamate. 6 Namwambia Mwenyezi-Mungu, “Wewe ndiwe Mungu wangu.” Usikilize, ee Mwenyezi-Mungu, sauti ya ombi langu. 7 Ee Mwenyezi-Mungu, Bwana wangu, mkombozi wangu mkuu, umenikinga salama wakati wa vita. 8 Ee Mwenyezi-Mungu, usiwape waovu wanayotaka; wala mipango yao mibaya usiifanikishe. 9 Hao wanaonizingira wanainua vichwa; uovu wa maneno yao uwapate wao wenyewe! 10 Makaa ya moto yawaangukie; watumbukizwe mashimoni, wasiinuke tena. 11 Wanaowasengenya wengine wasifanikiwe katika nchi; uovu uwapate wakatili na kuwaangamiza mara! 12 Najua Mwenyezi-Mungu hutetea kisa cha wanaoteswa, na kuwapatia haki maskini. 13 Hakika waadilifu watalisifu jina lako; wanyofu watakaa kwako.