132
Sifa ya nyumba ya Mungu(Wimbo wa Kwenda Juu) 1 Ee Mwenyezi-Mungu, mkumbuke Daudi, kumbuka taabu zote alizopata. 2 Ukumbuke ahadi aliyokupa, ee Mwenyezi-Mungu, kiapo alichokuapia, ewe Mwenye Nguvu wa Yakobo: 3 “Sitaingia ndani ya nyumba yangu, wala kulala kitandani mwangu; 4 sitakubali kulala usingizi, wala kusinzia; 5 mpaka nikupatie wewe Mwenyezi-Mungu mahali pa kukaa, makao yako, ewe Mwenye Nguvu wa Yakobo!” 6 Huko Efratha tulisikia habari za sanduku la agano, tukalikuta katika mashamba ya Yearimu. 7 “Haya! Twende nyumbani kwa Mungu, tuabudu mbele ya kiti chake cha enzi!” 8 Inuka ee Mwenyezi-Mungu, nenda kwenye maskani yako; inuka pamoja na sanduku la agano la uwezo wako! 9 Makuhani wako wawe waadilifu daima; na waaminifu wako wapige vigelegele vya furaha! 10 Kwa ajili ya Daudi, mtumishi wako, usimkatae huyo mfalme uliyemweka wakfu. 11 Mwenyezi-Mungu alimwapia Daudi kiapo thabiti, kiapo ambacho hatakibatilisha: “Nitamtawaza mmoja wa wazawa wako mwenyewe, kuwa mfalme baada yako. 12 Watoto wako wakishika agano langu, na kuzingatia mafundisho nitakayowapa, watoto wao pia watakuwa wafalme kama wewe.” 13 Mwenyezi-Mungu ameuchagua mji wa Siyoni, ametaka uwe makao yake: 14 “Hapa ndipo nitakapokaa milele, ndipo maskani yangu maana nimepachagua. 15 Nitaubariki sana mji wa Siyoni kwa mahitaji yake; nitawashibisha chakula maskini wake. 16 Nitawafanikisha makuhani wake kwa wokovu; waaminifu wake watapiga vigelegele vya furaha. 17 Humo nitamchipusha mfalme shujaa wa ukoo wa Daudi: Kama taa iwakayo nitamtegemeza mfalme niliyemteua. 18 Maadui zake nitawavika aibu; lakini yeye nitamvika fahari ya kifalme.”