30
Sala ya shukrani(Zaburi ya Daudi) 1 Ee Mwenyezi-Mungu, nakutukuza maana umeniokoa, wala hukuwaacha maadui zangu wanisimange. 2 Ee Mwenyezi-Mungu, Mungu wangu, nilikulilia msaada, nawe ukaniponya. 3 Ee Mwenyezi-Mungu, umeniokoa kutoka kuzimu; umenipa tena uhai, umenitoa miongoni mwa waendao kuzimu. 4 Mwimbieni Mwenyezi-Mungu sifa, enyi waaminifu wake; kumbukeni utakatifu wake na kumshukuru. 5 Hasira yake hudumu kitambo kidogo, wema wake hudumu milele. Kilio chaweza kuwapo hata usiku, lakini asubuhi huja furaha. 6 Mimi nilipofanikiwa, nilisema: “Kamwe sitashindwa!” 7 Kwa wema wako, ee Mwenyezi-Mungu, umeniimarisha kama mlima mkubwa. Lakini ukajificha mbali nami, nami nikafadhaika. 8 Nilikulilia wewe, ee Mwenyezi-Mungu; naam niliomba dua kwako ee Mwenyezi-Mungu: 9 “Je, utapata faida gani nikifa na kushuka hadi kwa wafu? Je, mavumbi ya wafu yanaweza kukusifu? Je, yanaweza kusimulia uaminifu wako? 10 Usikie, ee Mwenyezi-Mungu, unihurumie; ee Mwenyezi-Mungu, unisaidie!” 11 Wewe umegeuza maombolezo langu kuwa ngoma ya furaha; umeniondolea huzuni yangu, ukanizungushia furaha. 12 Mimi nitakusifu wala sitakaa kimya. Ee Mwenyezi-Mungu, Mungu wangu nitakushukuru milele.