85
Kuliombea fanaka taifa(Kwa Mwimbishaji. Zaburi ya Wakorahi) 1 Ee Mwenyezi-Mungu, umeifadhili nchi yako; umemjalia Yakobo bahati nzuri tena. 2 Umewasamehe watu wako kosa lao; umezifuta dhambi zao zote. 3 Umeizuia ghadhabu yako yote; umeiacha hasira yako kali. 4 Uturekebishe tena, ee Mungu mwokozi wetu; uiondoe chuki uliyo nayo juu yetu. 5 Je, utatukasirikia hata milele? Je, utadumisha ghadhabu yako kwa vizazi vyote? 6 Je, hutatujalia tena maisha mapya, ili watu wako wafurahi kwa sababu yako? 7 Utuoneshe, fadhili zako, ee Mwenyezi-Mungu, utujalie wokovu wako. 8 Hebu nisikie anachosema Mwenyezi-Mungu; maana anaahidi kuwapa watu wake amani, watu wake mwenyewe wasiporudia upuuzi wao 9 Hakika yu tayari kuwaokoa wanaomheshimu, na utukufu wake utadumu nchini mwetu. 10 Fadhili zake na uaminifu vitakutana; uadilifu na amani vitaungana. 11 Uaminifu utachipuka katika nchi; uadilifu utashuka toka mbinguni. 12 Naam, Mwenyezi-Mungu atatuletea fanaka, na nchi yetu itatoa mazao yake mengi. 13 Uadilifu utamtangulia Mungu na kumtayarishia njia yake.