46
Mungu yuko upande wetu(Kwa Mwimbishaji. Zaburi ya Wakorahi. Mtindo wa Alamothi) 1 Mungu ni kimbilio letu na nguvu yetu; yeye ni msaada wetu daima wakati wa taabu. 2 Kwa hiyo hatutaogopa chochote, dunia ijapoyeyuka na milima kutikisika kutoka baharini; 3 hata kama bahari ikichafuka na kutisha, na milima ikatetemeka kwa machafuko yake. 4 Kuna mto ambao maji yake hufurahisha mji wa Mungu, makao matakatifu ya Mungu Mkuu. 5 Mungu yumo mjini humo, nao hauwezi kutikiswa; Mungu ataupa msaada alfajiri na mapema. 6 Mataifa yaghadhibika na tawala zatikisika; Mungu anguruma nayo dunia yayeyuka. 7 Mwenyezi-Mungu wa majeshi yu pamoja nasi, Mungu wa Yakobo ni kimbilio letu. 8 Njoni mwone matendo ya Mwenyezi-Mungu; oneni maajabu aliyoyafanya duniani. 9 Hukomesha vita popote duniani, huvunjavunja pinde na mikuki, nazo ngao huziteketeza. 10 Asema: “Nyamazeni na kujua kuwa mimi ni Mungu! Mimi natukuka katika mataifa yote; mimi natukuzwa ulimwenguni kote!” 11 Mwenyezi-Mungu wa majeshi yu pamoja nasi, Mungu wa Yakobo ni kimbilio letu.