95
Utenzi wa kumsifu Mungu 1 Njoni tumwimbie Mwenyezi-Mungu, tumshangilie mwamba wa wokovu wetu! 2 Twende mbele zake na shukrani; tumshangilie kwa nyimbo za sifa. 3 Maana Mwenyezi-Mungu, ni Mungu mkuu; yeye ni Mfalme mkuu juu ya miungu yote. 4 Vilindi vyote vya dunia vimo mikononi mwake, vilele vya milima ni vyake. 5 Bahari ni yake, ndiye aliyeifanya; kwa mikono yake aliiumba nchi kavu. 6 Njoni tusujudu na kumwabudu; tumpigie magoti Mwenyezi-Mungu, Muumba wetu! 7 Maana yeye ni Mungu wetu, nasi ni watu wa kundi lake, ni kondoo wake anaowachunga. Laiti leo mngesikiliza sauti yake: 8 “Msiwe wakaidi kama kule Meriba, kama walivyokuwa kule Masa jangwani, 9 wazee wenu waliponijaribu na kunipima, ingawa walikuwa wameona mambo niliyowatendea. 10 Kwa miaka arubaini nilichukizwa nao, nikasema: ‘Kweli, hawa ni watu waliopotoka! Hawajali kabisa njia zangu!’ 11 Basi, nilikasirika, nikaapa: ‘Hawataingia mahali pangu pa pumziko!’”