41
Sala ya mgonjwa(Kwa Mwimbishaji. Zaburi ya Daudi) 1 Heri mtu anayewajali maskini; Mwenyezi-Mungu atamwokoa wakati wa shida. 2 Mwenyezi-Mungu atamlinda na kumweka hai, naye atafanikiwa katika nchi; Mungu hatamwacha makuchani mwa maadui zake. 3 Mwenyezi-Mungu atamsaidia awapo mgonjwa, atamponya maradhi yake yote. 4 Nami nilisema: “Unifadhili, ee Mwenyezi-Mungu, unihurumie maana nimekukosea wewe.” 5 Madui zangu husema vibaya juu yangu: “Atakufa lini na jina lake litoweke!” 6 Wanitembeleapo husema maneno matupu; wanakusanya mabaya juu yangu, na wafikapo nje huwatangazia wengine. 7 Wote wanichukiao hunongonezana juu yangu; wananiwazia mabaya ya kunidhuru. 8 Husema: “Maradhi haya yatamuua; hatatoka tena kitandani mwake!” 9 Hata rafiki yangu wa moyoni niliyemwamini, rafiki ambaye alishiriki chakula changu, amegeuka kunishambulia! 10 Ee Mwenyezi-Mungu, unionee huruma! Unipe nafuu, nami nitawalipiza. 11 Hivyo nitajua kwamba unapendezwa nami, maadui zangu wasipopata fahari juu yangu. 12 Wewe umenitegemeza kwani natenda mema; waniweka mbele yako milele. 13 Asifiwe Mwenyezi-Mungu, Mungu wa Israeli, tangu milele na hata milele! Amina! Amina!