62
Mungu mlinzi wangu(Kwa Mwimbishaji: Mtindo wa Yeduthuni. Zaburi ya Daudi) 1 Namngojea Mungu peke yake kwa utulivu, kwake watoka wokovu wangu. 2 Yeye peke yake ndiye mwamba na wokovu wangu, yeye ni ngome yangu, sitatikisika. 3 Hata lini mtanishambulia mimi? Hata lini nyinyi nyote mtanipiga, mimi niliye kama kiambaza kilichoinama, kama ukuta unaoanza kubomoka? 4 Mmepanga kuniangusha toka mahali pangu pa heshima; furaha yenu ni kusema uongo. Kwa maneno, mnabariki, lakini moyoni mnalaani. 5 Namngojea Mungu peke yake kwa utulivu; kwake naliweka tumaini langu. 6 Yeye peke yake ndiye mwamba na wokovu wangu, yeye ni ngome yangu, sitatikisika. 7 Wokovu na fahari yangu vyatoka kwa Mungu; mwamba wangu mkuu na kimbilio langu ni Mungu. 8 Enyi watu, mtumainieni Mungu daima; mfungulieni Bwana yaliyo moyoni mwenu. Mungu ndiye kimbilio la usalama wetu. 9 Binadamu wote ni kama pumzi tu; wote, wakubwa kwa wadogo, hawafai kitu. Tena ukiwapima uzito hawafikii kilo, wote pamoja ni wepesi kuliko pumzi. 10 Msitegemee dhuluma, msijisifie mali ya wizi; kama mali zikiongezeka, msizitegemee. 11 Mungu ametamka mara moja, nami nimesikia tena na tena: Kwamba enzi ni mali yake Mungu; 12 naam, nazo fadhili ni zake Bwana; humlipa kila mtu kadiri ya matendo yake.