81
Wimbo wa sikukuu(Kwa Mwimbishaji: Mtindo wa Gitithi. Zaburi ya Asafu) 1 Mwimbieni kwa sauti Mungu, nguvu yetu, mshangilieni Mungu wa Yakobo; 2 vumisheni wimbo wa shangwe, pigeni ngoma, chezeni zeze na kinubi cha sauti nzuri. 3 Pigeni tarumbeta kutangaza mwezi mwandamo, na pia mwezi mpevu, wakati wa sikukuu yetu. 4 Hiyo ndiyo kanuni katika Israeli; hilo ndilo agizo la Mungu wa Yakobo. 5 Aliwapa watu wa Israeli agizo hilo, alipoishambulia nchi ya Misri. Nasikia sauti nisiyoitambua ikisema: 6 “Mimi nilikutua mizigo yako mabegani, nilikuondolea matofali uliyochukua mikononi. 7 Ukiwa shidani uliniita, nami nikakuokoa. Nilikujibu nikiwa mafichoni katika ngurumo. Nilikujaribu kwenye maji ya Meriba. 8 Enyi watu wangu, sikieni onyo langu. Laiti ungenisikiliza, ee Israeli! 9 Asiwepo kwako mungu wa kigeni; usiabudu kamwe mungu mwingine. 10 Mimi ndimi Mwenyezi-Mungu, Mungu wako, niliyekutoa katika nchi ya Misri. Fumbua kinywa chako, nami nitakulisha. 11 “Lakini watu wangu hawakunisikiliza; Israeli hakunitaka kabisa. 12 Hivyo, nikawaacha wabaki na ukaidi wao; wafuate mashauri yao wenyewe. 13 Laiti watu wangu wangenisikiliza! Laiti Israeli angefuata njia yangu! 14 Ningewashinda maadui zao haraka; ningenyosha mkono dhidi ya wadhalimu wao. 15 Wanichukiao wangenipigia magoti kwa hofu, na adhabu yao ingekuwa ya milele. 16 Lakini wewe ningekulisha kwa ngano bora, ningekushibisha kwa asali ya mwambani.”