143
Sala ya kuomba msaada(Zaburi ya Daudi) 1 Usikie sala yangu, ee Mwenyezi-Mungu! Ulitegee sikio ombi langu maana wewe ni mwaminifu; unijibu kwa sababu ya uadilifu wako. 2 Usinitie hukumuni mimi mtumishi wako, maana hakuna yeyote aliye mwadilifu mbele yako. 3 Maadui zangu wamenifuatia; wameniangusha chini kabisa wameniketisha gizani kama mtu aliyekufa zamani. 4 Nimevunjika moyo kabisa; nimekufa ganzi kwa ajili ya woga. 5 Nakumbuka siku zilizopita; natafakari juu ya yote uliyotenda, nawaza na kuwazua juu ya matendo yako. 6 Nakunyoshea mikono yangu kuomba; nina kiu yako kama nchi kavu isiyo na maji. 7 Ee Mwenyezi-Mungu, unijibu haraka; maana nimekata tamaa kabisa! Usijifiche mbali nami, nisije nikawa kama wale washukao kwa wafu. 8 Asubuhi unioneshe fadhili zako, maana nimekuwekea tumaini langu. Unifundishe mwenendo wa kufuata, maana nakuelekezea ombi la moyo wangu. 9 Uniokoe, ee Mwenyezi-Mungu, kutoka maadui zangu, maana kwako nakimbilia usalama. 10 Unifundishe kutimiza matakwa yako, maana wewe ni Mungu wangu! Roho yako nzuri iniongoze katika njia sawa. 11 Unifadhili, ee Mwenyezi-Mungu, kwa hisani yako, uniondoe katika taabu kwa sababu ya uadilifu wako. 12 Kwa sababu ya fadhili zako uwakomeshe maadui zangu, uwaangamize wote wanaonidhulumu; maana mimi ni mtumishi wako.