32
Maondoleo ya dhambi(Zaburi ya Daudi. Funzo) 1 Heri yake mtu aliyesamehewa kosa lake, mtu ambaye dhambi yake imeondolewa kabisa. 2 Heri mtu ambaye Mwenyezi-Mungu hamwekei hatia, mtu ambaye hana hila moyoni mwake. 3 Wakati nilipokuwa sijakiri dhambi yangu, nilikuwa nimedhoofika kwa kulia mchana kutwa. 4 Mchana na usiku mkono wako ulinilemea; nikafyonzwa nguvu zangu, kama maji wakati wa kiangazi. 5 Kisha nilikiri makosa yangu kwako; wala sikuuficha uovu wangu. Nilisema ninakuungamia makosa yangu ee Mwenyezi-Mungu, ndipo nawe ukanisamehe dhambi zangu zote. 6 Kwa hiyo, kila mwaminifu na akuletee maombi; jeshi likaribiapo au mafuriko, hayo hayatamfikia yeye. 7 Wewe ndiwe kinga yangu; wewe wanilinda katika taabu. Umenijalia shangwe za kukombolewa. 8 Mungu asema: “Nitakufunza na kukuonesha njia unayopaswa kufuata. Nitakushauri kwa uangalifu mkubwa. 9 Usiwe mpumbavu kama farasi au nyumbu, ambao lazima wafungwe lijamu na hatamu, la sivyo hawatakukaribia.” 10 Watu waovu watapata mateso mengi, bali wanaomtumainia Mwenyezi-Mungu wazungukwa na fadhili zake. 11 Furahini na kushangilia kwa sababu ya Mwenyezi-Mungu enyi waadilifu; pigeni vigelegele vya shangwe enyi wanyofu wa moyo.